" MAADHIMISHO YA WIKI YA WAZAZI KATAVI YAFANYIKA MPANDA, MWENYEKITI WA JUMUIYA YA WAZAZI KATAVI ASISITIZA MALEZI BORA NA UZALENDO

MAADHIMISHO YA WIKI YA WAZAZI KATAVI YAFANYIKA MPANDA, MWENYEKITI WA JUMUIYA YA WAZAZI KATAVI ASISITIZA MALEZI BORA NA UZALENDO

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Katavi, Evarist Simon Mnyere, ameongoza maadhimisho ya Wiki ya Wazazi Mkoa wa Katavi yaliyofanyika Wilaya ya Mpanda Mei 7, 2026, huku akisisitiza umuhimu wa malezi bora na uzalendo katika kujenga taifa imara.

Katika maadhimisho hayo yaliyowakutanisha viongozi na wanachama wa Jumuiya ya Wazazi kutoka maeneo mbalimbali ya mkoa huo, Mnyere alisema wazazi wana wajibu mkubwa wa kushirikiana katika malezi ya watoto na vijana ili kuhakikisha jamii inapata viongozi bora wa baadaye.

Akizungumza katika hafla hiyo, aliwahimiza wazazi kuwaunganisha watoto katika ngazi mbalimbali za elimu kuanzia shule za msingi, sekondari, vyuo vya kati hadi vyuo vikuu, kwa lengo la kuwajengea misingi ya maadili, uzalendo na uwajibikaji.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa wazazi kushiriki shughuli za maendeleo na malezi mema katika jamii huku wakitekeleza kwa vitendo sera za malezi na makuzi ya watoto.

Mnyere pia aliwataka wazazi kuendelea kutunza mazingira, kuzingatia masuala ya afya, pamoja na kuimarisha maadili ya taifa kwa kuendeleza umoja na mshikamano ndani ya jumuiya hiyo.

Katika hatua nyingine, aliwashukuru wanachama wa Jumuiya ya Wazazi pamoja na viongozi wa chama na serikali kwa ushirikiano wanaoutoa katika kuimarisha jumuiya hiyo na kutekeleza shughuli mbalimbali za maendeleo.

Pia aliwahimiza wanachama kuendelea kubuni miradi ya maendeleo, kufanya mikutano ya mara kwa mara, kuweka takwimu sahihi za wanachama na kuimarisha nidhamu pamoja na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kauli mbiu ya maadhimisho hayo ilikuwa isemayo, “Malezi Bora na Uzalendo ni Msingi wa Taifa,” ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha jamii kuwekeza katika maadili na malezi ya watoto kwa maendeleo ya taifa.

Ndg. Evarist Simon Mnyere, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Katavi na Mgeni Rasmi wa maadhimisho ya Wiki ya Wazazi Mkoa wa Katavi, amewasili na kuwasalimia wanachama pamoja na wananchi katika eneo la Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo, Wilaya ya Mpanda, akiwa katika mwendelezo wa shughuli za maadhimisho hayo.
Ndg. Evarist Simon Mnyere, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Katavi na Mgeni Rasmi wa maadhimisho ya Wiki ya Wazazi Mkoa wa Katavi katika Wilaya ya Mpanda (Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo), ameungana katika picha ya pamoja na madaktari wakati wa maadhimisho hayo, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ushirikiano kati ya viongozi na sekta ya afya katika kuendeleza huduma kwa jamii.

 

 

Post a Comment

Previous Post Next Post