" BILIONI 25 ZAWEKEZWA UJENZI WA JENGO LA MAMA NA MTOTO HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA WA SHINYANGA, MKANDARASI AAHIDI KUKAMILISHA KWA WAKATI

BILIONI 25 ZAWEKEZWA UJENZI WA JENGO LA MAMA NA MTOTO HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA WA SHINYANGA, MKANDARASI AAHIDI KUKAMILISHA KWA WAKATI

Serikali imekabidhi rasmi eneo la ujenzi wa Jengo la Mama na Mtoto la ghorofa tano pamoja na Jengo la Maabara ya Kisasa la ghorofa mbili katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, mradi unaotarajiwa kugharimu zaidi ya shilingi bilioni 25 na kukamilika ndani ya kipindi cha miaka miwili.

Makabidhiano hayo yaliyohusisha utoaji wa Hati ya Makabidhiano ya Eneo la Ujenzi (Site Possession Certificate) yamefanyika Juni 5, 2026 katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, yakifungua rasmi utekelezaji wa mradi huo mkubwa wa kuboresha huduma za afya mkoani humo.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano hayo, Mshauri Mwelekezi kutoka Kampuni ya Volumetric Arch Consultant Ltd, Berno Batinamani, amesema mkandarasi ataanza rasmi kazi za ujenzi Juni 19, 2026 na mradi huo unatarajiwa kukamilika mwaka 2028.

Amesema kukamilika kwa majengo hayo kutasaidia kuongeza uwezo wa hospitali kutoa huduma za kisasa za afya kwa wananchi wa Mkoa wa Shinyanga na mikoa jirani, hususan katika huduma za afya ya mama na mtoto pamoja na huduma za uchunguzi wa maabara.

Kwa upande wake, Meneja wa Mkataba wa mradi huo kutoka Wizara ya Afya, Festo Mapunda, amemtaka mkandarasi kuhakikisha anatekeleza mradi kwa ubora unaotakiwa, ndani ya muda uliopangwa na kwa kuzingatia thamani halisi ya fedha za umma.

Mapunda pia amesisitiza matumizi ya nguvu kazi kutoka Mkoa wa Shinyanga ili wananchi waweze kunufaika na fursa za ajira zitakazotokana na mradi huo.

Naye Mkurugenzi wa Kampuni ya AMAR Builders Ltd, mkandarasi anayetekeleza mradi huo, Vipul Maran, amesema kampuni yake imejipanga kikamilifu kuhakikisha kazi zote zinakamilika kwa wakati na kwa kuzingatia viwango vya kitaalamu.

Amesema tayari maandalizi muhimu ya awali yamekamilika na kwamba wataendelea kushirikiana kwa karibu na Serikali pamoja na mshauri mwelekezi ili kuhakikisha mradi huo unatekelezwa kwa mafanikio makubwa.

Akizungumza kwa niaba ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Dkt. John Luzila, ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwekeza katika sekta ya afya.

Dkt. Luzila amesema Jengo la Mama na Mtoto litakuwa na uwezo wa kuhudumia wagonjwa 162 kwa wakati mmoja, hatua itakayosaidia kupunguza msongamano wa wagonjwa na kuboresha huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto katika Mkoa wa Shinyanga.

Aidha, amesema Jengo jipya la Maabara ya Kisasa lenye ghorofa mbili litasaidia kuboresha huduma za uchunguzi wa magonjwa na vipimo mbalimbali vya kitabibu, hivyo kuwapunguzia wananchi gharama na muda wa kusafiri kutafuta huduma hizo katika maeneo mengine.

Ameeleza kuwa mradi huo ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha miundombinu ya afya nchini kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora, za kisasa na zinazokidhi mahitaji ya wakati.

Wadau waliohudhuria hafla hiyo wameeleza matumaini yao kuwa mradi huo utakuwa miongoni mwa miradi itakayobadilisha kwa kiasi kikubwa huduma za afya katika Mkoa wa Shinyanga na maeneo ya jirani mara utakapokamilika.

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, Dkt. John Luzila akizungumza.





 SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment

Previous Post Next Post