" MCHUNGAJI KANONI JACKSON ISEKE WA KANISA LA ANGLIKANA SOLWA KASHISHI ASTAAFU UTUMISHI WA KICHUNGAJI, ASKOFU CHINYONG'OLE AMSIHI KUENDELEA KUWA MSHAURI WA KANISA

MCHUNGAJI KANONI JACKSON ISEKE WA KANISA LA ANGLIKANA SOLWA KASHISHI ASTAAFU UTUMISHI WA KICHUNGAJI, ASKOFU CHINYONG'OLE AMSIHI KUENDELEA KUWA MSHAURI WA KANISA


Na Mapuli Kitina Misalaba

Kanisa la Anglikana Solwa Kashishi la Dayosisi ya Shinyanga limefanya ibada maalum ya kumstaafisha Mchungaji Kanoni Jackson Daudi Iseke baada ya kulitumikia Kanisa kwa miaka mingi katika nafasi mbalimbali za uongozi wa kiroho.

Ibada hiyo iliyofanyika Juni 7, 2026 katika Kanisa la Anglikana Solwa Kashishi ilihudhuriwa na Askofu wa Dayosisi ya Shinyanga, Mhashamu Johnson Japheth Chinyong'ole, viongozi mbalimbali wa Kanisa, waumini pamoja na familia ya Mchungaji Kanoni Jackson Iseke.

Ibada hiyo iliongozwa na Katibu wa Dayosisi ya Shinyanga, Noel Bahati, huku historia fupi ya maisha na utumishi wa Mchungaji Kanoni Jackson Iseke ikisomwa na Shemasi Jefta Stanford Riniga.

Akihubiri katika ibada hiyo, Askofu Johnson Japheth Chinyong'ole alimpongeza Mchungaji Kanoni Jackson Iseke kwa uaminifu wake katika kulitumikia Kanisa na kumweleza kuwa kustaafu kwake ni mwisho wa nafasi ya kiuongozi lakini si mwisho wa utumishi wake kwa Mungu.

Askofu Chinyong'ole alisema kuwa Kanisa bado linahitaji hekima, ushauri na uzoefu wa viongozi waliolitumikia kwa muda mrefu, hivyo Mchungaji Iseke ataendelea kuwa mshauri muhimu kwa Kanisa, viongozi na waumini.

"Umeacha nafasi ya uongozi kwa mujibu wa taratibu za Kanisa, lakini bado wewe ni mtumishi wa Mungu. Tunaamini utaendelea kuwa mshauri na mfano bora kwa kizazi kinachoendelea na kazi ya Injili," alisema Askofu Chinyong'ole.

Kwa upande wake, Mchungaji Kanoni Jackson Iseke pamoja na familia yake walimshukuru Mungu kwa kuwawezesha kufika hatua hiyo ya ustaafu salama na kuwashukuru viongozi wa Kanisa, waumini, ndugu na marafiki kwa ushirikiano walioupata katika kipindi chote cha utumishi wake.

Baadhi ya viongozi na waumini wa Kanisa hilo waliopata nafasi ya kuzungumza walieleza kuwa Mchungaji Iseke ameacha alama kubwa katika maendeleo ya Kanisa la Solwa Kashishi, wakibainisha kuwa wakati anaanza kulitumikia eneo hilo hakukuwa na maendeleo makubwa ya miundombinu ya Kanisa, lakini kwa ushirikiano wa waumini na uongozi wake, hatua mbalimbali za maendeleo ikiwemo ujenzi wa Kanisa zimefanikiwa.

Kwa mujibu wa historia iliyosomwa, Mchungaji Kanoni Jackson Daudi Iseke alizaliwa Julai 1, 1954 katika Kitongoji cha Nhwiga, Kijiji cha Kabiga, Kata ya Kakola. Katika maisha yake ya utumishi amehudumu katika nafasi mbalimbali ikiwemo Mhazini wa Parishi ya Kakola, Mwinjilisti wa Parishi ya Nyang'ombe, Shemasi, Kasisi na baadaye kuhamishiwa Parishi ya Solwa Kashishi mwaka 2015.

Mwaka 2017 alipandishwa Daraja la Ukanoni na Askofu Johnson Japheth Chinyong'ole kutokana na mchango wake katika kuhubiri Injili na kuimarisha huduma za Kanisa.

Ibada hiyo ilihitimishwa kwa sala za shukrani na kumuombea Mchungaji Kanoni Jackson Daudi Iseke afya njema, amani na baraka za Mungu katika maisha yake ya ustaafu huku akiendelea kuwa nguzo ya ushauri kwa Kanisa na jamii kwa ujumla.

Askofu Johnson Japheth Chinyong'ole akitoa mahubiri na nasaha mbalimbali kwa Mchungaji Kanoni Jackson Daudi Iseke pamoja na waumini waliohudhuria ibada hiyo.

Katibu wa Dayosisi ya Shinyanga, Noel Bahati, akiongoza ibada maalum ya kustaafu kwa Mchungaji Kanoni Jackson Daudi Iseke.


 SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA

Post a Comment

Previous Post Next Post