" SHIRIKA LA KIVULINI LAENDELEA KUIMARISHA AFYA YA MAMA NA MTOTO KUPITIA MRADI WA GROW ENRICH KATIKA WILAYA YA SHINYANGA

SHIRIKA LA KIVULINI LAENDELEA KUIMARISHA AFYA YA MAMA NA MTOTO KUPITIA MRADI WA GROW ENRICH KATIKA WILAYA YA SHINYANGA

Shirika la Kivulini linaendelea kutekeleza mradi wa GROW ENRICH unaolenga kuboresha afya ya mama na mtoto pamoja na kuongeza ushiriki wa wanaume katika masuala ya afya ya familia. Mradi huu unatekelezwa kwa ushirikiano na Shirika la World Vision Tanzania, ukiwa na lengo la kupunguza vifo vya wajawazito na watoto wachanga kupitia elimu, ushirikishwaji wa jamii na uimarishaji wa huduma za afya.

Katika utekelezaji wa mradi huo, Shirika la Kivulini limefanya midahalo ya kijamii katika Kata za Mwalukwa na Usanda, zilizopo Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. Midahalo hiyo iliwakutanisha wananchi, viongozi wa serikali, wataalamu wa afya na watumishi wa Shirika la Kivulini ili kujadili changamoto zinazoikabili afya ya mama na mtoto pamoja na kuweka mikakati ya pamoja ya kuzitatua.

Kata ya Mwalukwa: Jamii Yapata Elimu na Kuweka Maazimio ya Mabadiliko

Mdahalo uliofanyika Kata ya Mwalukwa ulifanikiwa kwa kiwango kikubwa ambapo wananchi walipata elimu mbalimbali kuhusu afya ya uzazi, malezi na umuhimu wa ushiriki wa baba katika afya ya familia.

Akizungumza katika mdahalo huo, Meneja wa Mradi wa GROW ENRICH, Mageni Malulu, alisema kuwa mradi huo unafanya kazi kwa karibu na vituo vya afya na zahanati kwa kuwajengea uwezo watumishi wa afya pamoja na wahudumu wa afya ngazi ya jamii ili kuboresha huduma zinazotolewa kwa mama na mtoto.

"Mradi huu unalenga kuhakikisha vifo vya mama na mtoto vinapungua. Pia tumekuwa tukianzisha vikundi mbalimbali ndani ya jamii ikiwemo vikundi vya Baba Bora, vinavyowahamasisha wanaume kushiriki kikamilifu katika huduma za afya ya familia na malezi ya watoto," alisema Malulu.

Aliongeza kuwa vikundi hivyo vinaendelea kuwafikia wanaume wengi zaidi na kuwawezesha kuwa sehemu ya maamuzi na huduma zinazohusu afya ya familia.

 

Polisi Jamii Watoa Elimu Dhidi ya Ukatili wa Kijinsia

Katika mdahalo huo, Jeshi la Polisi kupitia kitengo cha Polisi Jamii lilishiriki kutoa elimu kuhusu kupinga ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto.

Polisi walisisitiza kuwa baba ana wajibu wa kuwa mlinzi wa familia yake kwa kuhakikisha anazuia vitendo vya ukatili na kujenga mazingira salama kwa wanawake na watoto.

Aidha, Koplo Gabriel alitumia sanaa ya uimbaji kuelimisha wananchi kuhusu madhara ya ukatili wa kijinsia pamoja na umuhimu wa kuzingatia sheria na usalama barabarani, jambo lililowavutia wananchi wengi na kufanya ujumbe kufika kwa urahisi.

Bodaboda Wakabidhiwa Vizibao vya Elimu

Katika kuongeza wigo wa kufikisha ujumbe kwa jamii, madereva wa bodaboda walikabidhiwa vizibao vyenye ujumbe wa kuhamasisha ushiriki wa baba katika afya ya mama na mtoto.

Hatua hiyo inalenga kuhakikisha ujumbe unaendelea kuwafikia wananchi wengi zaidi kupitia bodaboda ambao hukutana na watu wengi katika shughuli zao za kila siku.

Sababu Zinazochangia Ushiriki Mdogo wa Baba

Mdahalo ulioongozwa na Afisa Maendeleo wa Kata ya Mwalukwa, Elipendo John, uliwapa wananchi nafasi ya kueleza changamoto zinazowafanya baadhi ya wanaume kushindwa kushiriki kikamilifu katika afya ya mama na mtoto.

Baadhi ya sababu zilizotajwa ni:

  • Mila na desturi zinazotafsiri huduma za afya ya uzazi kuwa ni jukumu la wanawake pekee.
  • Ukosefu wa elimu kuhusu nafasi ya baba katika afya ya familia.
  • Majukumu ya kiuchumi na shughuli za kutafuta kipato.
  • Hofu au aibu ya kwenda kliniki pamoja na wenza wao.
  • Mawasiliano hafifu kati ya wanandoa kuhusu masuala ya afya ya uzazi.

Baada ya mjadala huo, wananchi waliweka maazimio ya pamoja yatakayofuatiliwa ili kuongeza ushiriki wa wanaume katika afya ya familia.

Elimu ya Lishe Yaongeza Uelewa wa Jamii

Afisa Lishe aliyeshiriki mdahalo huo alitoa elimu kuhusu umuhimu wa lishe bora kwa mama mjamzito, mama anayenyonyesha na mtoto.

Alisisitiza kuwa baba ana nafasi muhimu katika kuhakikisha familia inapata lishe bora kwa:

  • Kushiriki kupanga na kununua vyakula vyenye virutubisho.
  • Kumsaidia mama wakati wa ujauzito na kipindi cha kunyonyesha.
  • Kuhamasisha mahudhurio ya kliniki kwa mama na mtoto.
  • Kushiriki malezi ya mtoto tangu kuzaliwa.
  • Kuweka mazingira yanayomwezesha mama kupata mapumziko na huduma stahiki.

Michezo Yatumika Kufikisha Ujumbe wa Afya

Shughuli hiyo ilipambwa na burudani mbalimbali ikiwemo mashindano ya mpira wa miguu ambapo wanaume wa kijiji waligawanywa katika timu za Simba na Yanga.

Mashindano hayo yaliwavutia wananchi wengi kujitokeza kushuhudia mchezo huo. Wakati wa mapumziko, wataalamu walitoa elimu kuhusu afya ya mama na mtoto pamoja na umuhimu wa baba kushiriki katika malezi na afya ya familia. Baada ya mchezo kuendelea na kumalizika, mdahalo uliendelea huku elimu ikiendelea kutolewa kwa wananchi waliohudhuria.

Kata ya Usanda: Mashindano ya Baiskeli Yavutia Wananchi

Utekelezaji wa shughuli uliendelea katika Kata ya Usanda ambapo ulianza kwa mashindano ya baiskeli yaliyowashirikisha wanaume kutoka katika jamii.

Mashindano hayo yaliwavutia wananchi wengi kujitokeza, hali iliyotoa fursa nzuri ya kufikisha ujumbe wa mradi kwa idadi kubwa ya watu.

Baada ya mashindano hayo, mdahalo ulifanyika ukiongozwa na Afisa Maendeleo, Afisa Lishe, Mwenyekiti wa Kijiji pamoja na maafisa kutoka Shirika la Kivulini.

Wananchi walipata elimu kuhusu afya ya mama na mtoto, umuhimu wa ushiriki wa baba katika malezi na huduma za afya, huku wakikubaliana kwa pamoja maazimio mbalimbali yatakayosaidia kuongeza ushiriki wa wanaume katika afya ya familia.

Aidha, madereva wa bodaboda katika kata hiyo walikabidhiwa vizibao vyenye ujumbe maalumu wa kuhamasisha ushiriki wa baba katika malezi na afya ya mama na mtoto ili ujumbe huo uendelee kuwafikia wananchi wengi zaidi.

Wananchi Wanufaika na Huduma za Afya Bure

Mbali na midahalo na utoaji wa elimu, shughuli zote zilizofanyika katika Kata za Mwalukwa na Usanda ziliambatana na utoaji wa huduma za afya bila malipo kwa wananchi. Huduma hizo zilitolewa na wataalamu wa afya kwa lengo la kuongeza upatikanaji wa huduma za kinga na uchunguzi wa mapema wa magonjwa mbalimbali.

Wananchi walipata fursa ya kupimwa Virusi vya UKIMWI (VVU), kiwango cha wingi wa damu (Hemoglobin), magonjwa ya zinaa pamoja na vipimo vingine vya msingi vya afya kulingana na mahitaji. Aidha, huduma za ushauri nasaha zilitolewa kwa wananchi ili kuwasaidia kufanya maamuzi sahihi kuhusu afya zao, afya za wenza wao na ustawi wa familia kwa ujumla.

Huduma hizo zilihamasisha wananchi wengi kujitokeza kupima afya zao, kupata ushauri kutoka kwa wataalamu na kuelewa umuhimu wa uchunguzi wa afya wa mara kwa mara. Kupitia huduma hizi, Mradi wa GROW ENRICH umeendelea kuhamasisha jamii kuchukua hatua za mapema katika kulinda afya ya mama, mtoto na familia kwa ujumla.

 

Kupitia Mradi wa GROW ENRICH, Shirika la Kivulini linaendelea kushirikiana na serikali, wataalamu wa afya na jamii kuhakikisha afya ya mama na mtoto inaendelea kuimarika huku likihamasisha wanaume kuwa washiriki muhimu katika malezi na ustawi wa familia.

Kupitia midahalo, elimu, michezo na ushirikishwaji wa wadau mbalimbali, mradi huu unaendelea kujenga jamii yenye uelewa mkubwa zaidi kuhusu afya ya familia na kuchangia kupunguza vifo vya mama na mtoto katika Wilaya ya Shinyanga.

 SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment

Previous Post Next Post