" MGEJA AWAHIMIZA WAHITIMU OLD SHINYANGA KUJIFUNZA UFUGAJI, ASEMA DUNIA HAIHITAJI VYETI PEKEE

MGEJA AWAHIMIZA WAHITIMU OLD SHINYANGA KUJIFUNZA UFUGAJI, ASEMA DUNIA HAIHITAJI VYETI PEKEE


Mwenyekiti wa Chama cha Msalaba Mwekundu Tanzania (TRCS) Mkoa wa Shinyanga, Hatibu Madata Mgeja, amewahimiza wahitimu kutumia kipindi cha mapumziko baada ya kumaliza mitihani yao kujifunza ujuzi mbalimbali wa maisha, ikiwemo ufugaji, akisisitiza kuwa dunia ya sasa haihitaji vyeti vya darasani pekee.


Mgeja ametoa kauli hiyo Agosti 27, 2026, akiwa mgeni rasmi katika mahafali ya 19 ya Kidato cha Nne ya Shule ya Sekondari Old Shinyanga, na kwamba amewasisitiza wahitimu kujituma, kuwa na nidhamu, utiifu na kuendelea kutafuta maarifa nje ya yale waliyofundishwa darasani.

Amesema baada ya kumaliza mitihani yao, vijana watakuwa na kipindi cha mapumziko ambacho wanapaswa kukitumia kujifunza shughuli mbalimbali za uzalishaji na kujenga ujuzi ambao unaweza kuwasaidia katika maisha yao ya baadaye.

“Hivi karibuni mtaenda kufanya mitihani yenu ya mwisho, baada ya mtihani mtakuwa na mapumziko ya miezi kadhaa. Tumieni kipindi hicho kutafuta maarifa nje ya yale mliyofundishwa shuleni, jifunzeni ufugaji wa kuku na ng’ombe. Mimi ni mfugaji, nitawakaribisha shambani kwangu mje mjifunze,” amesema Mgeja.

Mgeja amesema dunia ya sasa ina fursa nyingi ambazo zinaweza kuwawezesha vijana kujenga maisha yao hata pale wanaposhindwa kuendelea na masomo, hivyo amewaasa wahitimu kuwa wabunifu na kutumia fursa zinazowazunguka.

Mgeja pia amewataka wahitimu hao kuwa mabalozi wa amani, uzalendo na kuipenda nchi yao, huku akiwaasa kujiepusha na watu wanaopenda vurugu na fujo.

Amesema Tanzania ni moja na hivyo vijana wana wajibu wa kulinda amani, umoja na mshikamano wa taifa, akiwataka kutumia elimu na maarifa yao kwa manufaa ya jamii.

Katika mahafali hayo, Mgeja ameupongeza uongozi wa shule, walimu na wafanyakazi wasio walimu kwa juhudi wanazofanya katika kusimamia taaluma na maadili ya wanafunzi.

Pia amewapongeza wazazi wa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Old Shinyanga kwa kutoa ushirikiano katika kuhakikisha watoto wao wanapata mahitaji muhimu wanapokuwa shuleni, hususan chakula.

Mgeja ametoa ahadi mbalimbali kwa shule hiyo, ikiwemo kutoa seti za jezi za mpira, pamoja na tanki la maji, huku pia akiahidi kuchangia shilingi 600,000 katika ujenzi wa miundombinu ya shule.

Kwa upande wake, kaimu Afisa Elimu sekondari Manispaa ya Shinyanga Beatrice Senzighe Mbonea  amewataka wahitimu kutumia elimu waliyoipata shuleni kama msingi wa kuendelea kujifunza na kujenga maisha yao.

Mbonea amesisitiza umuhimu wa kuwa na nidhamu, kujituma, kuheshimu wazazi na walezi pamoja na kutumia maarifa waliyojifunza kwa manufaa yao binafsi na jamii kwa ujumla.

Akizungumza katika mahafali hayo, Mkuu wa Shule ya Sekondari Old Shinyanga, Marco Msangwa Itenga, amesema shule hiyo inakabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo ukosefu wa kisima cha maji, uzio wa shule kwa ajili ya kuimarisha usalama na usimamizi wa nidhamu ya wanafunzi, matanki ya kuhifadhia maji pamoja na upungufu wa nyumba za walimu.

Amesema shule hiyo ina jumla ya wanafunzi 1,282, wakiwemo wavulana 884 na wasichana 408, huku ikiwa na jumla ya walimu 34.

Katika matokeo ya Kidato cha Nne ya mwaka 2025, shule hiyo ilikuwa na wanafunzi 130 waliopata madaraja mbalimbali, ambapo wanafunzi 9 walipata Daraja la Kwanza, 16 Daraja la Pili, 52 Daraja la Tatu na 53 Daraja la Nne.

Itenga amesema ni matumaini ya uongozi wa shule kwamba wanafunzi wanaotarajia kufanya mtihani wao wa mwisho wa Kidato cha Nne mwezi Novemba 2026 watafanya vizuri zaidi.

Amesema shule hiyo pia imeendelea kufanya vizuri katika taaluma, ikiwemo kushika nafasi ya kwanza kati ya shule 16 katika mtihani wa Mock Kanda uliofanyika Novemba 2025.

Katika risala yake, Mkuu wa Shule ametoa shukrani kwa Serikali kupitia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa fedha zilizotolewa kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya shule.

Ametaja shilingi milioni 342.9 zilizotolewa mwaka 2025 kwa ajili ya ujenzi wa Shule ya Awali na Msingi Butulwa, shilingi milioni 25 kwa ajili ya ukarabati wa vyumba viwili vya madarasa, pamoja na shilingi milioni 31 zilizotolewa kwa ajili ya ukarabati wa vyumba viwili vya madarasa, jengo la utawala, viunga vya shule na jengo la maabara.

Mahafali hayo ya 19 yamewakutanisha viongozi, walimu, wazazi, walezi na wanafunzi, huku Mgeni Rasmi, Hatibu Madata Mgeja, akiwahimiza wahitimu kuendelea kuthamini elimu, kujenga nidhamu na kutumia maarifa na fursa zilizopo katika jamii kwa ajili ya maisha yao ya baadaye.

Mgeni Rasmi, Hatibu Madata Mgeja, akizungumza wakati wa Mahafali ya 19 ya Kidato cha Nne ya Shule ya Sekondari Old Shinyanga, akiwahimiza wahitimu kutumia muda wao kujifunza ujuzi mbalimbali wa maisha.  

Mgeni Rasmi, Hatibu Madata Mgeja, akiwa katika picha ya pamoja.



 

SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment

Previous Post Next Post