Mbio za
Mwenge wa Uhuru zinatarajiwa kuwasili Mkoani Shinyanga Agosti 19, 2026,
ukitokea Mkoani Mwanza na kupokelewa katika Kata ya Kolandoto, huku ukitarajiwa
kukimbizwa jumla ya kilomita 84.8 ndani ya Manispaa ya Shinyanga.
Mkurugenzi
wa Manispaa ya Shinyanga Mwl. Alexius Kagunze
amesema Mwenge huo
utatumika kufikia miradi mbalimbali ya maendeleo kwa ajili ya kuzinduliwa,
kuwekwa mawe ya msingi, kufunguliwa na kukaguliwa, pamoja na kutoa elimu kwa
wananchi kuhusu masuala mbalimbali ya kijamii na kiuchumi.
Miongoni mwa
miradi hiyo ni mradi wa upanuzi wa mtandao wa maji Kolandoto, ambao
utazinduliwa mara baada ya mapokezi ya Mwenge, pamoja na shughuli katika Zahanati
ya Mwasalele zinazohusisha huduma za afya na elimu kwa wananchi.
Kwa mujibu
wa Mkurugenzi huyo, Mwenge pia utafika Makindo Royal Hotel, ambako kutawekwa jiwe
la msingi la mradi wa uwekezaji wa sekta binafsi, kabla ya kuelekea katika eneo
la mradi wa nishati kwa ajili ya uzinduzi na uhamasishaji kuhusu matumizi
sahihi ya nishati.
Aidha,
Mwenge utafikia Daraja la Dodoma, ambako kutafanyika ufunguzi wa daraja hilo,
hatua inayolenga kuboresha usafiri na mawasiliano kwa wananchi.
Katika sekta
ya elimu, Mwenge utafika Shule ya Sekondari Rajani na Shule ya Sekondari Old
Shinyanga, ambako pamoja na shughuli za ujumbe wa Mwenge, wananchi
watahamasishwa kuhusu umuhimu wa elimu na ushiriki wa jamii katika kuboresha
mazingira ya kujifunzia.
Mkurugenzi
huyo amesema pia Mwenge utafika Kata ya Kambarage, katika eneo la Mkesha wa
Mwenge wa Uhuru Kitaita, ambako utakagua na kuzindua shughuli za vijana pamoja
na mabanda yanayotoa elimu kuhusu dawa za kulevya, uchangiaji wa damu salama,
lishe, rushwa na VVU/UKIMWI.
Aidha, vikundi
vya vijana na shughuli zao za kiuchumi vitakaguliwa kwa lengo la kuhamasisha
vijana kutumia fursa za kujiajiri na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya
jamii.
Kwa ujumla,
Mkurugenzi amesema ziara hiyo inalenga kuhamasisha wananchi kuhusu maendeleo,
afya, elimu, maji, nishati, miundombinu, uwekezaji, uwezeshaji wa vijana na
uwajibikaji, huku wananchi wakihimizwa kushiriki katika kusimamia miradi
inayotekelezwa katika maeneo yao.
Mwenge wa
Uhuru unatarajiwa kukabidhiwa kwa viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya
Shinyanga Agosti 20, 2026, katika Shule ya Msingi Tinde A, baada ya kukamilisha
safari yake ya kilomita 84.8.
SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254
Post a Comment