" VIJANA 120 WAHITIMISHA MIAKA 22 YA HUDUMA YA MTOTO NA KIJANA SHINYANGA, MAASKOFU WATOA NASAHA KWA VIJANA

VIJANA 120 WAHITIMISHA MIAKA 22 YA HUDUMA YA MTOTO NA KIJANA SHINYANGA, MAASKOFU WATOA NASAHA KWA VIJANA

Jumla ya vijana 120 wamehitimisha rasmi safari yao ya miaka 22 ndani ya Huduma ya Mtoto na Kijana Klas­ta ya Shinyanga, katika hafla iliyofanyika Septemba 5, 2026, huku viongozi wa dini wakitoa wito kwa vijana kuendelea kumcha Mungu, kuthamini elimu na kutumia fursa walizopata kuleta mabadiliko katika jamii.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa dini, serikali, wazazi, walezi, watendaji wa huduma ya mtoto na kijana, pamoja na wadau wa maendeleo.

Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Baba Askofu wa Kanisa Anglikana, Mheshimiwa Johnson Chinyong'ole, ambaye aliungana na Askofu wa AICT Dayosisi ya Shinyanga,  Zakayo Bugota, katika kutoa nasaha na kuwatia moyo vijana hao wanaofungua ukurasa mpya wa maisha yao.

Miaka 22 ya malezi, elimu na kumjua Mungu

Akielezea safari yao, vijana hao walisema miaka 22 ndani ya huduma hiyo imekuwa zaidi ya kipindi cha kukua; imekuwa safari ya malezi, elimu, afya, ulinzi, maadili na kumjua Mungu.

Walisema walipoanza safari hiyo wakiwa watoto wadogo, wengi walikuwa na ndoto ambazo hawakujua kama zingetimia, lakini kupitia huduma hiyo walipata watu wa kuwashika mkono, kuwaelekeza na kuwaamini.

“Tumekuwa, tumele­lewa, tumesoma, tumetibiwa, tumefundishwa maadili mema na tumemjua Mungu.”

Kwa mujibu wa risala yao, elimu waliyoipata haikuishia katika kupata vyeti, bali iliwawezesha kujenga uwezo wa kufanya maamuzi sahihi, kuwajibika, kujitegemea na kuwa na mchango katika jamii.

Baadhi yao wamefanikiwa kuwa mainjinia, walimu, wahasibu, mafundi, wafanyabiashara na wajasiriamali, huku wengine wakiendelea kujenga taaluma na maisha yao.

Compassion International yatambuliwa kwa mchango wake

Katika hafla hiyo, vijana hao pia walitambua mchango wa Compassion International katika safari yao ya miaka 22, wakieleza kuwa ushirikiano kati ya kanisa na shirika hilo umechangia kuwapa watoto na vijana fursa ya kukua na kustawi kwa mtazamo mpana.

Huduma hiyo imegusa maeneo mbalimbali ikiwemo elimu, afya, malezi, ulinzi wa mtoto, mahitaji ya msingi, makuzi ya kijamii na kihisia pamoja na malezi ya kiroho.

Vijana hao walitoa shukrani kwa Compassion International kwa kuamini katika maisha yao na kueleza kuwa mchango walioupokea haujaishia kwenye kile walichopokea, bali unaonekana pia katika kile walichokua na kile wanachotarajia kuwa katika siku zijazo.

Wito wa kulinda watoto dhidi ya ukatili

Mbali na kusherehekea mafanikio yao, vijana hao walitumia hafla hiyo kutoa wito kwa serikali, kanisa na jamii kwa ujumla kuendelea kushirikiana katika kuhakikisha watoto wanakua katika mazingira salama.

Walitaja changamoto zinazohitaji kuendelea kupigwa vita, ikiwemo ukatili na unyanyasaji wa watoto, ndoa na mimba za utotoni, ajira hatarishi kwa watoto, ukosefu wa elimu na unyanyasaji wa kingono.

Aidha, walitoa wito kwa jamii kutoa taarifa pale mtoto anapokabiliwa na mazingira yanayoweza kuhatarisha maisha, afya, usalama na mustakabali wake.

Ujumbe kwa vijana wanaoendelea na huduma

Vijana hao waliowahi kuwa sehemu ya huduma hiyo pia walitoa ujumbe maalumu kwa vijana ambao bado wanaendelea na huduma ya mtoto na kijana.

Walihimiza vijana hao kutokata tamaa, kusoma kwa bidii, kumjua Mungu, kuheshimu wazazi, walezi, kanisa na watendaji wa huduma, huku wakisisitiza umuhimu wa kulinda ushuhuda wao.

Walitoa ushuhuda kwamba wao wenyewe ni mfano wa namna mtoto anapopewa nafasi, upendo, ulinzi na elimu anaweza kukua na kuwa kijana mwenye mchango mkubwa katika jamii.

“Ndoto zenu zinawezekana kutimia. Sisi tulio hapa leo ni ushahidi kwamba mtoto akipewa nafasi anaweza kusoma, kuwa na afya njema, kumjua Mungu na kuwa chachu ya mabadiliko katika jamii.”

Maaskofu wawahimiza vijana kuitumia nafasi waliyopewa

Katika hafla hiyo, Baba Askofu Johnson Chinyong'ole pamoja na Askofu Zakayo Bugota walitoa nasaha kwa vijana, wakiwahimiza kutambua thamani ya malezi na fursa walizopata, kumtegemea Mungu katika hatua mpya ya maisha na kutumia elimu na ujuzi wao kwa manufaa ya jamii.

Ujumbe wa viongozi hao ulienda sambamba na wito wa vijana hao wenyewe kwamba mafanikio waliyoyapata yasibaki kuwa historia yao binafsi, bali yawe msingi wa kuwainua wengine.

“Baraka tulizopokea zinapaswa kuwa baraka kwa wengine”

Wakihitimisha risala yao, vijana hao walisema wanaingia katika hatua mpya ya maisha wakiwa na jukumu la kutumia elimu, malezi na maadili waliyopata kwa manufaa ya kanisa na jamii.

Walisisitiza kuwa wataendelea kuwa mabalozi wa amani na ulinzi wa mtoto, na pale watakapopata nafasi ya kuwasaidia wengine, watafanya hivyo kwa sababu wamejifunza kuwa:

“Baraka tulizopokea zinapaswa kuwa baraka kwa wengine pia.”

Hafla hiyo imekuwa alama muhimu kwa vijana hao 120, ambao baada ya miaka 22 ya safari ndani ya Huduma ya Mtoto na Kijana wamehitimisha rasmi hatua hiyo wakiwa na kumbukumbu, elimu, malezi na matumaini ya kuendelea kujenga maisha yenye kusudi.

Mungu awabariki vijana wote waliohitimu na awape hekima na nguvu katika safari yao mpya ya maisha.


Mgeni rasmi, baba Askofu wa Kanisa Anglikana, Mheshimiwa Johnson Chinyong'ole, akizungumza. 

Askofu wa AICT Dayosisi ya Shinyanga,  Zakayo Bugota, akizungumza.




Post a Comment

Previous Post Next Post