" TAMASHA LA UTAMADUNI LA 19 LAFANYIKA JIGOKU, MWENYEKITI WA MACHIFU TANZANIA CHIFU ANTONIA SANGALALI ATOA UJUMBE KUHUSU AMANI, ELIMU NA MILA

TAMASHA LA UTAMADUNI LA 19 LAFANYIKA JIGOKU, MWENYEKITI WA MACHIFU TANZANIA CHIFU ANTONIA SANGALALI ATOA UJUMBE KUHUSU AMANI, ELIMU NA MILA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Tamasha la 19 la Himaya ya Jigoku (Masela), Wilaya ya Maswa mkoani Simiyu, likiongozwa na Mwenyekiti wa Machifu Tanzania na Mtemi wa Himaya ya Jigoku, Chifu Antonia Sangalali, limehamasisha amani, maadili na uendelezaji wa mila na desturi za Kitanzania.

Akizungumza katika tamasha hilo, Chifu Sangalali amesema matamasha hayo yataendelea kufanyika kila mwaka kwa lengo la kuendeleza mila na tamaduni za Kitanzania, kutoa burudani na kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa amani na maadili.

Amesema matamasha hayo pia ni sehemu ya kuimarisha mshikamano na kupunguza uhalifu katika jamii, huku akiwataka wananchi kuendelea kuiheshimu Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuweka amani mbele.

“Tutaendelea kuwaletea matamasha haya kila mwaka yakiambatana na ngoma za asili ili tuburudike. Hii ni sehemu ya kupunguza uhalifu. Tuendelee kuiheshimu Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tuendelee kuiweka amani mbele na maadili tuyafuate ili tuweze kuishi kwa amani,” amesema Chifu Sangalali.

Katika tamasha hilo, Chifu Sangalali pia ametoa ujumbe wa Benki Kuu ya Tanzania kwa wananchi kuhusu utunzaji wa noti, akiwataka kutokuzichana, kuzitoboa wala kuziandikia kwa kuwa fedha hizo hutumiwa na watu mbalimbali.

Aidha, amewataka wananchi kuchukua tahadhari dhidi ya uwezekano wa mvua za El Niño, ikiwemo kutunza chakula na kuondoka katika maeneo hatarishi endapo kutatokea mvua kubwa na mafuriko.

Chifu Sangalali pia ametoa wito kwa wanafunzi, hususan wasichana, kuzingatia elimu na kutokukimbilia ndoa kabla ya kukamilisha masomo yao.

Kwa upande wake, mgeni rasmi katika tamasha hilo, Mkuu wa Wilaya ya Maswa, Dkt. Vicent Anney, amempongeza Chifu Antonia Sangalali kwa kuendeleza tamasha hilo kila mwaka, akisema ni sehemu muhimu ya kuhifadhi historia ya machifu nchini Tanzania.

Amehimiza wananchi kuendelea kulinda amani, mshikamano, mila na desturi za Kitanzania, akisisitiza kuwa taifa haliwezi kuwa bora bila kuheshimu na kuhifadhi utamaduni wake.

Mkuu huyo wa Wilaya amewataka pia vijana kuwa mstari wa mbele katika kulinda amani na mshikamano katika jamii na kuepuka vitendo vinavyoweza kuvuruga amani.

Baadhi ya wakazi wa Himaya ya Jigoku wamempongeza Chifu Antonia Sangalali kwa kuendelea kuandaa tamasha hilo kila mwaka, wakisema limekuwa likiwapa fursa ya kukutana, kuburudika pamoja na kupata elimu na ujumbe mbalimbali kuhusu maisha ya jamii.

Tamasha hilo pia limewakutanisha ndugu wa utemi wa Chifu Sangalali kutoka maeneo mbalimbali, ikiwemo Dar es Salaam, Dodoma na Kagera, pamoja na wageni kutoka nchini Uganda.

Burudani mbalimbali za ngoma za asili zimetawala katika tamasha hilo, huku msanii maarufu wa ngoma za asili, Shule ya Ng’ombe, akiongoza kutoa burudani na kuifanya siku  kuwa ya kipekee kwa washiriki.

Mwenyekiti wa Machifu Tanzania na Mtemi wa Himaya ya Jigoku, Chifu Antonia Sangalali ni mmoja wa waazilishi wa matamasha hayo yanayowakutanisha machifu na jamii, hivyo ametumia nafasi hiyo kuhimiza kuendelea kuyafanya kwa kuwa ni sehemu ya kuhifadhi historia, mila na tamaduni za Kitanzania.

Mwenyekiti wa Machifu Tanzania na Mtemi wa Himaya ya Jigoku, Chifu Antonia Sangalali, akizungumza wakati wa Tamasha la Utamaduni la 19 la Himaya ya Jigoku, Maswa mkoani Simiyu.

 

Post a Comment

Previous Post Next Post