" WANANCHI SHINYANGA WAOMBA ELIMU KUHUSU TAHADHARI ZA MVUA ZA EL NINO

WANANCHI SHINYANGA WAOMBA ELIMU KUHUSU TAHADHARI ZA MVUA ZA EL NINO

Na Edington Ezron, Misalaba Media

Baadhi ya wananchi katika Manispaa ya Shinyanga wameiomba serikali na mamlaka husika kuendelea kutoa elimu kuhusu tahadhari zinazopaswa kuchukuliwa kuelekea msimu wa mvua zinazotarajiwa kuwa na athari kwa makazi ya watu, mifugo na maisha ya wananchi.

Wananchi hao kutoka katika mitaa mbalimbali ya Manispaa ya Shinyanga wameyasema hayo kwa nyakati tofauti walipokuwa wakizungumza na Misalaba Media, ambapo wameeleza umuhimu wa kuchukua tahadhari mapema ili kuepusha madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na mvua hizo.

Mmoja wa wananchi hao, Elias Masanja, amesema kila mwananchi anapaswa kuchukua hatua za kujikinga na athari za mvua hizo hususani kwa wakazi wanaoishi katika maeneo ya mabonde.

Kwa upande wake, Michael Peter amesema wananchi hawapaswi kupuuza taarifa na tahadhari zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), akisema baadhi ya watu wamekuwa wakizichukulia taarifa hizo kama jambo la kawaida, hali inayoweza kusababisha madhara makubwa.

Aidha, wananchi hao wameiomba serikali kushirikiana nao katika kuboresha miundombinu ya kupitisha maji, ikiwemo ujenzi wa mifereji na mitaro, ili kupunguza hatari ya mafuriko katika makazi ya watu.

Naye Mwenyekiti wa Mtaa wa Miti Mirefu, Nassoro Warioba, amesema wameanza mchakato wa kuzibua mitaro katika baadhi ya maeneo ya mtaa huo, huku wakiendelea na jitihada za kurekebisha maeneo yenye changamoto, ikiwemo karavati lililopo katika barabara ya Mwanza–Mkabara na Shy Pazuri.

Warioba ameongeza kuwa serikali ya mtaa inaendelea kutoa elimu kwa wananchi wanaoishi katika maeneo hatarishi, ikiwemo maeneo ya Mto Buluba na maeneo mengine yenye changamoto.

Amewasihi wananchi kuchukua hatua za mapema, ikiwemo kuziba madimbwi ya maji, ili kupunguza uwezekano wa kutokea kwa mafuriko na madhara mengine yanayoweza kusababishwa na mvua hizo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mtaa wa Mwinamila, Juma Athuman Mboma, amewasihi wananchi kuzingatia usalama wao wakati wa mvua, ikiwemo kuepuka kutembea wakati mvua kubwa inanyesha ili kujikinga na hatari ya kupigwa na radi au kusombwa na maji.

Pia ameiomba serikali kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kutoa ushirikiano kwa wananchi kwa kujenga mitaro ya kupitisha maji na kuyaelekeza katika maeneo salama yasiyo na makazi ya watu.

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa tahadhari kwa wananchi kuhusu uwezekano wa mvua kubwa katika kipindi kijacho, huku ikiwataka kuendelea kufuatilia taarifa rasmi za hali ya hewa na kuchukua tahadhari mapema ili kujikinga na athari zinazoweza kujitokeza, ikiwemo mafuriko, upepo mkali na radi.

 SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment

Previous Post Next Post