" UONGOZI MPYA RED CROSS SHINYANGA WAKUTANA NA KATIBU TAWALA, WAWEKA MKAKATI WA KUKABILIANA NA MAAFA IKIWEMO EL NINO

UONGOZI MPYA RED CROSS SHINYANGA WAKUTANA NA KATIBU TAWALA, WAWEKA MKAKATI WA KUKABILIANA NA MAAFA IKIWEMO EL NINO

Uongozi mpya wa Shirika la Msalaba Mwekundu Tanzania (Red Cross) Mkoa wa Shinyanga umefanya kikao na Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga, Pili Mnyema, kwa lengo la kujitambulisha rasmi pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya shirika hilo na Serikali katika kutoa huduma za kibinadamu kwa wananchi.

Kikao hicho pia kimejikita katika kujadili namna ya kuimarisha ushirikiano katika masuala ya maafa, majanga, uokoaji, huduma za dharura na utoaji wa misaada kwa wananchi pindi yanapotokea majanga mbalimbali katika Mkoa wa Shinyanga.

Akizungumza katika kikao hicho, Mwenyekiti wa Red Cross Mkoa wa Shinyanga, Hatibu Mgeja, amempongeza Katibu Tawala wa Mkoa, Pili Mnyema, kwa kuendelea kuaminiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kupewa jukumu la kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga.

Mgeja amemkaribisha Katibu Tawala huyo mkoani Shinyanga na kumhakikishia kuwa uongozi mpya wa Red Cross uko tayari kutoa ushirikiano wa karibu kwa Serikali katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma muhimu, hususani wakati wa majanga na changamoto zinazohitaji mwitikio wa haraka.

Amesema Red Cross ina nafasi muhimu katika kusaidia jamii wakati wa majanga, hivyo ushirikiano na Serikali ni jambo la msingi katika kuhakikisha maandalizi na mwitikio wa majanga unakuwa wa haraka na wenye ufanisi.

“Tunampongeza Katibu Tawala wa Mkoa kwa kuendelea kuaminiwa na Mheshimiwa Rais na tunamkaribisha rasmi Mkoani Shinyanga. Sisi kama Red Cross tupo tayari kutoa ushirikiano wa aina yoyote katika kuwatumikia wananchi wa Mkoa wa Shinyanga,” amesema Mgeja.

Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga, Pili Mnyema, amewashukuru viongozi wa Red Cross kwa kufika ofisini kwake katika siku ya kwanza akiwa katika ofisi yake kama Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga.

Mnyema amesema Serikali iko tayari kushirikiana na Red Cross katika utekelezaji wa majukumu yake, akisisitiza umuhimu wa kuwa na maandalizi ya pamoja katika kukabiliana na majanga yanayoweza kujitokeza.

Amesema ushirikiano huo ni muhimu zaidi katika kipindi ambacho kuna tahadhari kuhusu uwezekano wa mvua kubwa zinazoweza kusababisha changamoto mbalimbali ikiwemo mafuriko, uharibifu wa miundombinu na kuathiri maisha ya wananchi.

“Tunawashukuru wana-Red Cross kwa kuja kututembelea siku ya kwanza nikiwa ofisini kama Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga. Tutashirikiana nanyi kikamilifu, hasa katika kipindi hiki ambacho kuna tahadhari ya ujio wa mvua za El Nino,” amesema Mnyema.

Ameongeza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuhakikisha jamii inaelimishwa, inaandaliwa na inachukua tahadhari mapema ili kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na majanga.

Ushirikiano kati ya Serikali na Red Cross unatarajiwa pia kusaidia katika kuongeza uelewa wa jamii kuhusu utunzaji wa mazingira, tahadhari dhidi ya majanga, maandalizi ya kaya na namna ya kuchukua hatua za haraka wakati wa dharura.


Mwenyekiti wa Red Cross Mkoa wa Shinyanga, Hatibu Mgeja, akizungumza kwenye kikao hicho ambapo amempongeza Katibu Tawala Pili Mnyema kwa kuendelea kuaminiwa na Rais na kumuahidi ushirikiano katika kuwatumikia wananchi.Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga, Pili Mnyema, amesema Serikali iko tayari kushirikiana na Red Cross katika kuhakikisha wananchi wanakuwa salama wakati wa majanga.

Uongozi mpya wa Red Cross Mkoa wa Shinyanga umekutana na Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga, Pili Mnyema, kwa lengo la kujitambulisha na kuimarisha ushirikiano katika huduma za kibinadamu na kukabiliana na majanga.

 








Picha ya pamoja.


 

Post a Comment

Previous Post Next Post