Na Mapuli Misalaba, Shinyanga
Katibu wa CCM wilaya ya Shinyanga Mjini Ally Bin Ally amewataka viongozi wa CCM Wilaya hiyo kuachana na siasa za makundi na badala yake wafanye kazi kwa umoja ili kuleta matokeo chanya yenye manufaa kwa wananchi.
Ameyasema hayo leo kwenye Mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye kata ya Masekelo Manispaa ya Shinyanga,ambao umeandaliwa na jumuiya ya umoja wa wanawake UWT wilaya ya Shinyanga Mjini ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Miaka 46 ya kuzaliwa kwa CCM.
Katibu wa CCM Wilaya ya Shinyanga mjini Ally Bin Ally jina maarufu Majeshi amesema kutimiza miaka 46 ya CCM viongozi wanapaswa kujitafakari kwa kuongeza juhudi kwenye siasa zenye tija na kwamba wasiwe chanzo cha migogoro na kutengeneza makundi mabaya na mbasuko ndani ya chama.
“Tunapoelekea kutimiza Miaka 46 bado ndani ya chama kuna wana CCM wanadhani chama kina miaka nane au tisa, bado ndani ya chama hiki tuna nongwa za uchaguzi wanaojaliwa kuteuliwa kupata ridhaa au nafasi za kupeperusha pendala wanafikiri wanapewa hati miliki ya hizo nafasi walizopewa au wao ndiyo watu sahihi ndani ya chama waache”.amesema Majeshi
“Tulipotoka mwaka 2019 tukaenda 2020 nongwa za ubunge zipo unapopewa nafasi ndani ya chama kwa tiketi ya chama cha mapinduzi hujamilikishwa chama maana yake viongozi wetu waliopewa nafasi wasifanye kazi ya kukigawa chama kwa sababu ya kwamba kwa kuwa wao wananafasi basi wale ambao waliomba nao nafasi basi wale ambao waliomba nao hiyo nafasi wasiwe na nafasi wala thamani na heshima ndani ya chama jambo hili siyo sahihi watu waache tabia ya kukifuruga chama kwa sababu ya tafsiri potofu ambazo anazo yeye binafsi”.amesema Majeshi
Akizungumza Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini Anord Makombe pamoja na mambo mengine amewataka viongozi wakiwemo watendaji pamoja na wenyeviti wa serikali za mitaa kuhakikisha wanafunzi wote waliochaguliwa kujiunga na kidato Cha Mwanza wanakwenda shuleni.
Makombe ameeleza kuwa serikali tayari imeboresha miundombinu katika sekta ya elimu kwa shule za msingi na sekondari hivyo watoto wote wanaotakiwa kuendelea na masomo wasizuiliwe kwa sababu sizizo za msingi.
Bwana Makombe amewasisita viongozi hao kushirikiana na jamii kuhakikisha watoto wote waliochaguliwa kujiunga na kidato Cha kwanza wanakwenda shule huku akiwaomba Walimu kutowarudisha wanafunzi kutokana na sababu zozote zile.
“Tunao wenyeviti wa mitaa tunao watendaji lakini pia tunao waheshimiwa madiwani itakuwa ni jambo la ajabu serikali inawekeza miundombinu yakutosha kwenye elimu kuanzia shule ya msingi hadi sekondari halafu matokeo yake shule hizo zisiwe na watoto, tukute watoto wameishia mtaani kuzurula au kuuza karanga na kufanya biashara zisizo kuwa na sababu au maana yoyote ile mimi niwaase tuhakikishe kwamba watoto wote waliochaguliwa wanaenda shule hasa wale wa kidato cha kwanza, darasa la kwanza na chekechea”.amesema Makombe
Kwa upande wake Mwenyekiti wa UWT wilaya ya Shinyanga Mjini Rehema Nhamanilo ameeleza namna Jumuiya hiyo ilivyoshiriki katika maadhimisho hayo ambapo amesema wamefanya shughuli mbalimbali za kijamii ikiwemo kupanda miti katika maeneo tofauti ya Manispaa ya Shinyanga.
“Tumetembelea maeneo mbalimbali wanawake kamati ya utekelezaji tukishirikiana na kamati ya siasa ya wilaya tumefanya kazi nyingi tumekwenda kituo cha afya kambarage kusalimia wodi ya wazazi lakini pia tumeenda kituo cha watoto wenye uhitaji shule ya msingi Buhangija lakini pia tumeenda Hospitali yetu ya rufaa ya Mkoa tumepanda miti pamoja na Masekelo na Ndala”.amesema Rehema Nhamanilo
Jumuiya ya umoja wa wanawake wilaya ya Shinyanga mjini leo imeadhimisha Miaka 46 ya CCM Kwa kushiriki shughuli mbalimbali za kijamii ikiwemo kupanda miti 1210 na kutoa misaada ya sabuni na mafuta kwa wahitaji.
Wamepanda miti 407 eneo la Hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, miti 300 katika eneo la Masekelo sekondari, miti 203 eneo la Zahanati ya Masekelo, miti 200 eneo la Ndala sekondari pamoja na miti 100 eneo la Zahanati ya Ndala Manispaa ya Shinyanga.
Post a Comment