" DC SAMIZI AIPONGEZA PASS TRUST KWA KUENDELEA KUTOA DHAMANA YA MIKOPO KWA WAKULIMA

DC SAMIZI AIPONGEZA PASS TRUST KWA KUENDELEA KUTOA DHAMANA YA MIKOPO KWA WAKULIMA

 Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Johari Samizi, ameipongeza taasisi ya kusaidia sekta binafsi ya Kilimo (PASS TRUST) kwa namna inavyochochea maendeleo ya kilimo  kwa dhamana ya mikopo inayoitoa kwa wakulima, kupitia taasisi mbalimbali za kifedha.

Samizi ametoa pongezi hizo leo tarehe 20.04.2023, wakati akizungumza kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Shinyanga, katika ufunguzi wa warsha ya siku moja ya kuzindua Progromu ya KIJANISHA MAISHA katika mkoa wa Shinyanga, iliyokuwa imeandaliwa na PASS TRUST, iliyowashirikisha wadau mbalimbali wa sekta za kilimo, uvuvi, ufugaji na mazao ya misitu kutoka wilaya zote za mkoa wa Shinyanga.

Amepongeza ubunifu uliofanywa na taasisi hiyo kwa kuja na mbinu zinazowawezesha wakulima kuwekeza kwenye kilimo kinachoweza kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi, badala ya kubaki wakitegemea mvua za msimu, ambapo pia ametumia nafasi hiyo kuwataka wakulima wote kuhakikisha wanafanya shughuli zao kwa kuzingatia uhifadhi wa mazingira, ikiwemo kutokata miti ovyo na kuharibu vyanzo vya maji.

Samizi amebainisha kuwa, dhamana ya mikopo inayotolewa na taasisi hiyo kwa ajili ya wakulima na sekta nyingine zinazonufaika na mpango huo, inasaidia kwa kiasi kikubwa kuwezesha juhudi za Serikali ya awamu ya sita katika kuwainua wakulima wadogo, ili watoke kwenye kilimo cha kujikimu na badala yake waingie katika kilimo cha kibiashara (kilimobiashara)

Mkuu huyo wa Wilaya amezitaka taasisi za kifedha zilizoingia ubia na PASS  TRUST kutotumia fursa hiyo kuwaumiza wakulima, kwa kuwatoza kiwango kikubwa cha riba.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa maendeleo ya biashara wa PASS TRUST Bw. Adam Kamanda, amesema taasisi hiyo tangu kuanzishwa kwake mwaka 2000, imetoa dhamana ya mikopo yenye thamani ya Shilingi Trioni 1.3 kwa uwekezaji katika sekta za kilimo, uvuvi, ufugaji na mazo ya misitu, ambapo kwa kanda ya ziwa kwa mwaka uliopita wa 2022, imedhamini jumla ya mikopo yenye thamani ya Shilingi Bilioni 93.1, huku mkoa wa Shinyanga ukiwa umepata dhamana ya jumla ya Shilingi Bilioni 35.5.

Taasisi ya PASS TRUST, ilianzishwa mwaka 2000 na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Denimark kupitia mpango wa kuwezesha kilimo ili kusaidia uzalishaji wenye tija, ambapo chini ya mpango uliozinduliwa hivi karibuni wa KIJANISHA MAISHA, taasisi hiyo imejikita zaidi kudhamini miradi ambayo imelenga kuleta mageuzi kwenye sekta ya kilimo, ili iendane na sera ya uhifadhi wa mazingira.

Taasisi hiyo imeingia ubia wa kutoa dhamana ya mikopo kwa wakulima, wafugaji, wavuvi na waliowekeza kwenye mazao yatokanayo na misitu na taasisi 14 za kifedha, ikiwemo Benki za MKOMBOZI, NMB, NBC, CRDB na Vision Fund.

 

Post a Comment

Previous Post Next Post