" MGODI WA ALMAS MWADUI WALIPA FIDIA WAATHIRIKA WA TOPE BILIONI 1.8, UJENZI WA NYUMBA ZAO KUANZA JUNI.

MGODI WA ALMAS MWADUI WALIPA FIDIA WAATHIRIKA WA TOPE BILIONI 1.8, UJENZI WA NYUMBA ZAO KUANZA JUNI.


Na Stela Paul, Misalaba Blog

Mgodi wa Almas wa Williamson Mwadui unaomilikiwa na Kampuni ya Petra Diamonds Limited uliopo Wilaya ya Kishapu Mkoani Shinyanga mpaka sasa umelipa fidia ya shilingi bilioni 1.8 kwa waathirika wa tope.

Hayo ni kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana April 15,2023 na Meneja Mahusiano wa Mgodi huo Bernard Mihayo wakati akikabidhi fidia za samani za ndani kwa baadhi ya waathirika hao ikiwemo pikipiki, baiskel, chakula, mashine za umwagiliaji, vitanda pamoja na magodoro.

Amesema waathirika 294 kati ya 304 wameshalipwa fidia zao ambapo zoezi hilo litaendelea mpaka pale watakapokamilisha ulipaji wa fidia hizo.

" Tulikuwa na watu 304 na tayari tumeshawalipa watu 294 na hao ni katika upotevu wa mali aina mbalimbali ikiwemo ardhi, lakini kwa kaya kama hizi za leo wao walipoteza ardhi pamoja na nyumba,

"Kwa kuongezea waliopoteza nyumba, tutaanza mchakato wa kujenga nyumba zao Mwezi wa sita nyumba kama 47, na ukiangalia fidia yote mpaka Jana tumeshalipa shilingi bilioni 1 na milioni 800 na tunaendelea kulipa fidia. Na hiyo si pamoja na nyumba, nyumba zitakuwa na gharama yake tofauti" amesema Mihayo.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu Bi. Grace Mwandu amesema halmashauri imelipokea zoezi hilo kwa moyo wa dhati, huku akiwasihi waathirika wa tope kutumia fidia zao kwa ustawi bora wa maisha.

"Tumelipokea vizuri zoezi hili kwa sababu wananchi wote wamelizika na hakuna hata mmoja ambaye amekuwa na malalamiko dhidi ya mgodi huu, zaidi tu kwa wananchi ambao wamelipwa watumie fidia hizo kwa manufaa" amesema Grace.

Kwa upande wao wenyeviti wa vijiji vilivyoathirika na tope hilo, Mwenyekiti wa Kijiji cha Nyeze Revocatus Kulwa na Mwenyekiti wa kijiji cha Ng'wanholo William Kabisi wamepongeza jitihada mbalimbali ambazo zimefanywa na Mgodi huo ili kuhakikisha wananchi hao wanapata fidia zao ambapo pia wamethibitisha kuwa zoezi hilo linaendelea vizuri.

Nao baadhi ya wananchi waliolipwa fidia hizo wamepongeza na kuushukuru uongozi wa Mgodi wa Almas wa Williamson Mwadui kwa kutekeleza kwa wakati zoezi la ulipaji fidia.

Waathirika hao wametokana baada ya kingo za Bwawa la maji tope katika katika Mgodi huo kuvunjika Novemba 07, 2022 na kisha tope hilo kusambaa kwenye makazi ya watu wanaozunguka mgodi huo na kusababisha athari mbalimbali.

Meneja Mahusiano wa Mgodi wa Almasi Mwadui Benard Mihayo (kushoto) akikabidhi Fidia ya Jenereta kwa waathirika wa bwawa la tope la mgodi huo.

Post a Comment

Previous Post Next Post