" BENKI YA MAENDELEO YA KILIMO YATAKIWA KUWEZESHA WAKULIMA –WAZIRI BASHE

BENKI YA MAENDELEO YA KILIMO YATAKIWA KUWEZESHA WAKULIMA –WAZIRI BASHE

 Na Lucas Raphael, Misalaba Media -Tabora

Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe ameitaka Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB)  kuakikisha inatoa  ushauri pamoja na kuwajengea uwezo wakulima ili kuwezesha kuinuka kiuchumi    .

Alitoa kauli hiyo jana  wakati wa uzinduzi ofisi ya TADB Kanda ya Magharibi iliyofanyika katika viwanja wa benki hiyo  ambayo itatoa huduma katika Mikoa ya Tabora, Katavi na Kigoma.

Waziri Bashe alisema  kwamba  benki hiyo inawajibu mkubwa wa kuhakikisha inatoa elimu na ushauri nzuri kwa wakulima ili kupanua  wigo wa huduma zenye masharti nafuu na wezeshi kwa wakulima wadogo,  kati na wakubwa.

Alisema kwamba  upatikanaji wa mikopo nafuu kwa wakulima, wavuvi na wafugaji, utahamasisha zaidi ukuaji wa biashara katika mnyororo wa thamani kwenye mikoa itakayohudumia.

Waziri Bashe alitaka benki hiyo ya kilimo kutoa mikopo yenye masharti nafuu, kwa viwango vya riba za chini na kutoa muda mrefu zaidi wa marejesho kwa wakulima ili kuwezesha upatikanaji wa mitaji ya kuleta mapinduzi katika Sekta ya Kilimo.

Awali Mkurugenzi Mtendaji wa TADB,  Frank Nyabundege alimweleza Waziri Bashe kwamba katika  kipindi cha kuanzia Januari 2020 hadi Desemba, 2023, Benki ilitoa mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 516, kwa njia ya moja kwa moja (Direct Lending).

Alisema kwamba mikopo hiyo ili kwa ajili ya kuendeleza miradi ya kilimo, mifugo na uvuvi nchini.

Frank alieleza kwamba shilingi bilioni 448. kwenye Kilimo mazao, shilingi bilioni 60.43 zilitolewa kwenye mifugo, na shilingi bilioni 7.5 zilitolewa kwenye sekta ya Uvuvi.

Aliendelea kueleza kuwa  Mikopo hiyo ilitolewa kwenye miradi ya aina tofauti katika minyororo ya thamani 36 katika mikoa 27 na wilaya 125 na vyama vya wakulima 151.

Mkurungezi huyo aliendelea kusema kwamba hadi kufikia Februari, mwaka huu TADB imekwisha wezesha wakulima na wafugaji kwa kutoa mikopo yenye jumla ya thamani ya shilingi bilioni 19.5 ambapo Mkoa wa Kigoma walipatiwa kiasi cha shilingi bilion 7.2.

Aliongeze kusemakuwa  Mkoa wa Katavi,ulipatiwa kiasi cha s shilingi bilioni 2.394, na Mkoa wa Tabora, shilingi bilioni 9.996 mikopo hiyo ilitolewa kwenye miradi ya mpunga, chikichi, maharage, mahindi, unenepeshaji wa ng’ombe, tangawizi, ufugaji wa kuku, ufugaji wa nguruwe, na ufugaji wa kondoo.

Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Balozi Dkt. Batilda  Burian, alipongeza hatua hiyo muhimu ya kuleta huduma za Benki ya TADB katika Mikoa ya Tabora, Katavi na Kigoma na kueleza utakuwa  ni ukombozi kwa wakulima, wavuvi na wafugaji katika kukuza mitaji .

Post a Comment

Previous Post Next Post