Ticker

6/recent/ticker-posts

WAZIRI GWAJIMA ALANI MAUAJI YA MTOTO ASIMWE MWENYE UALBINO








Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima amelaani vikali mauaji ya mtoto Asimwe Novath mwenye umri wa miaka miwili na miezi sita, wa Kitongoji cha Mbale Kijiji cha Bulamula kata ya Kamachumu wilaya ya Muleba mkoani Kagera.

Waziri Gwajima ametoa kauli hiyo Juni 17, 2024 kupitia akaunti yake ya mtandao wa kijamii wa _Instagram_ kufuatia taarifa iliyotolewa na chombo kimoja cha Habari nchini kuwa mwili wa mtoto huyo mwenye ualbino umekutwa umefungwa kwenye mfuko (Sandarusi) huku ukiwa hauna baadhi ya viungo katika kijiji cha Malele.

“Walaaniwe wote wanaoamini kuwa viungo vya binadamu yeyote yule vina msaada kwenye maendeleo na ustawi wao. Watu hawa hawafai kwenye jamii. Nina Imani watapatikana hawa wauaji wakajibu kesi yao. Maafisa Maendeleo ya jamii na wote wenye mapenzi mema tushirikiane kwa nguvu zetu zote na akili zetu zote kuelimisha jamii kuachana na uovu huu. ” amesema Waziri Dkt. Gwajima.

“Asimwe Novath aliibwa nyumbani kwao Mei 30 mwaka huu, baada ya mama yake kukabwa na watu wasio julikana usiku wa saa 2:30 kisha mtoto huyo kuchukuliwa ambapo amekuwa akitafutwa hadi mwili wake ulipopatikana leo Juni 17, 2024, katika Kijiji cha Malele kata Ruhanga wilaya ya Muleba mkoani Kagera.” imesema sehemu ya taarifa hiyo.

Post a Comment

0 Comments