Na Mapuli Kitina Misalaba
Mwanamke mmoja anayefahamika kwa jina Mwajuma Shaban anashikiliwa
na Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga kwa tuhuma za kumwagia mafuta ya petroli
na kumchoma moto mume wake kufuatia mgogoro wa wivu wa mapenzi uliotokea katika
Mtaa wa Mageuzi, Kata ya Ngokolo, Manispaa ya Shinyanga.
Akizungumza na Misalaba Media, Kamanda wa Polisi Mkoa
wa Shinyanga, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP), amesema tukio hilo
lilitokea Machi 5, 2026 majira ya saa sita usiku.
Amesema majeruhi ametambulika kwa jina la David Mollis
mwenye umri wa Miaka 34, dereva wa bodaboda na mkazi wa Mtaa wa Mageuzi ambapo
inadaiwa kuwa wakati akiwa amekaa sebuleni nyumbani kwake, alijeruhiwa baada ya
kumwagiwa mafuta ya petroli na kuwashiwa moto na mke wake na kusababisha kupata
majeraha katika sehemu mbalimbali za mwili ikiwemo kifuani na mkononi.
Kwa mujibu wa Kamanda huyo, mwanamke anayehusishwa na
tukio hilo ni Mwajuma Shaban Mwenye umri wa Miaka 24 ambaye pia ni mkazi wa
mtaa huo na alikuwa akiishi pamoja na David kama mke na mume.
Amesema chanzo cha tukio hilo kinadaiwa kuwa ni wivu
wa mapenzi, ambapo mwanamke huyo alidai kuwa alimkopesha mume wake kiasi cha
shilingi 80,000 na baadaye kuhisi kuwa fedha hizo zimetolewa kwa mwanamke
mwingine.
Kamanda Magomi amesema kuwa majeruhi anaendelea
kupatiwa matibabu katika Hospitali ya Manispaa ya Shinyanga huku uchunguzi
ukiendelea ili mtuhumiwa aweze kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.
Kamanda huyo amelaani kitendo hicho na kutoa wito kwa
wanandoa na jamii kwa ujumla kuepuka vitendo vya ukatili na badala yake kutatua
migogoro kwa kufuata taratibu za kisheria.
Amesema Jeshi la Polisi lina madawati maalum
yanayoshughulikia ukatili wa kijinsia na kusisitiza kuwa ukatili unaweza
kuwakumba wanawake, watoto pamoja na wanaume.
Wakati huo huo, Misalaba Media imefika katika eneo la
tukio na kuzungumza na baadhi ya majirani wakiwemo wapangaji wenzake Cesilia
John, Lucy Shija pamoja na jirani Bi. Rosemary Mboje, ambao wamethibitisha
kutokea kwa tukio hilo majira ya saa sita usiku.
Majirani hao wamesema hawakuwa na taarifa ya mgogoro
wowote kati ya wanandoa hao kabla ya tukio hilo kutokea, ambapo wameeleza kuwa
baada ya tukio hilo walifanikiwa kumzuia mwanamke huyo ili asikimbie hadi jeshi
la Polisi lilipofika.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Wasafirishaji Bodaboda
Mitumbani Kata ya Ngokolo, Jacobo Msimbang’ombe, amesema amesikitishwa na tukio
hilo lililompata mwanachama wao na kuwataka madereva wa bodaboda kushirikishana
changamoto wanazokutana nazo ili kupata suluhisho kabla ya madhara makubwa
kutokea.
Naye Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Mageuzi,
Vitalis Mugisha, amesema alipigiwa simu na mmiliki wa nyumba aliyopanga David
na kufika katika eneo la tukio kabla ya kutoa taarifa kwa viongozi mbalimbali
ikiwemo Jeshi la Polisi ili hatua zaidi zichukuliwe.
Ametoa wito kwa wananchi kuacha tabia ya kujichukulia
sheria mkononi na badala yake kutumia njia za kisheria kutatua migogoro.
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment