" ICS NA ANGEL GABRIEL DAY CARE CENTER SHINYANGA WAUNGANA KUADHIMISHA SIKU YA KIMATAIFA YA MICHEZO

ICS NA ANGEL GABRIEL DAY CARE CENTER SHINYANGA WAUNGANA KUADHIMISHA SIKU YA KIMATAIFA YA MICHEZO

Ikiwa leo Juni 11, 2025 ni Siku ya Kimataifa ya Michezo kwa Watoto (International Day of Play), Shirika la ICS kwa kushirikiana na Angel Gabriel Day Care Center wameshiriki michezo ya pamoja iliyojumuisha watoto wa kituo hicho pamoja na wazazi wao, ikiwa ni sehemu ya kuenzi siku hiyo muhimu kwa ustawi wa mtoto.

Katika maadhimisho hayo yaliyofanyika mkoani Shinyanga, watoto wameshiriki michezo mbalimbali ya kufurahisha na kujenga, huku wazazi wakipata nafasi ya kushiriki kikamilifu pamoja na watoto wao.

Akizungumza afisa mradi kutoka shirika lisilo la kiserikali la Investing in Children and Strengtherning their Societies (ICS ) Lucy Maganga, amesema lengo la michezo hiyo ni kuimarisha ukaribu wa mzazi na mtoto, sambamba na kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa michezo katika malezi na makuzi ya awali ya mtoto.

 “Sisi kama ICS tuliona ni vizuri tushirikishe wadau wanaofanya kazi za moja kwa moja na watoto. Katika mkoa wa Shinyanga tunaratibu pia programu jumuishi ya malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto kwa watoto kuanzia umri wa miaka 0 hadi 8. Tumeona tushirikiane na Angel Gabriel Day Care kufanya jambo la maana kwa watoto wetu.”

Lucy ameongeza kuwa michezo kati ya mzazi na mtoto huimarisha mawasiliano ya karibu na hutoa nafasi kwa mtoto kueleza hisia zake kwa uhuru, ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa iwapo atakumbana na vitendo vya ukatili.

“Mzazi kucheza na mtoto siyo kupoteza muda, bali ni njia ya kujenga mahusiano yenye faida kubwa kwa baadaye,” amesisitiza Lucy Maganga.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Angel Gabriel Day Care Center, Bi. Damary Mollessi, amesema kuwa pamoja na watoto na wazazi kwa uchache wao, wamepata nafasi ya kujumuika na kushiriki michezo kama njia ya kukuza furaha, afya na vipaji vya watoto.

“Tumetoa elimu kwa wazazi juu ya umuhimu wa malezi bora, ikiwa ni pamoja na kucheza na watoto. Mtoto anayecheza anaweza kutambua kipaji chake mapema, na anapokua siyo rahisi kupata msongo wa mawazo kwani tayari ubongo wake umejengwa kukabiliana na changamoto,” amesema Bi. Damary.

Baadhi ya wazazi walioshiriki wamepongeza tukio hilo na kuahidi kuendeleza michezo na watoto wao majumbani, hasa wakati wa likizo, ili kuwakinga dhidi ya mazingira hatarishi na mmomonyoko wa maadili.

Nao baadhi ya watoto walioshiriki michezo hiyo, wameonyesha furaha yao kwa namna walivyoshiriki katika michezo mbalimbali, huku wakionekana wenye afya, shauku, na ujasiri wa kipekee.

Kwa wazazi wanaotafuta mahali salama na bora kwa watoto wao, Angel Gabriel Day Care inakaribisha watoto kujiunga kwa muhula wa pili unaoanza tarehe 8 Julai 2025.

Kaulimbiu ya kituo: “Making your child's world better.”

Kwa mawasiliano zaidi:
📞 0752 516 753 / 0675 969 213
📍Mwasele, Shinyanga

Mkurugenzi wa Angel Gabriel Day Care Center, Bi. Damary Mollessi akizungumza. 

 

Michezo mbalimbali ikiendelea kwenye kituo cha Angel Gabriel Day Care Center kilichopo Mwasele Manispaa ya Shinyanga, ikiwa ni sehemu ya maadhimishi ya Siku ya Kimataifa ya Michezo kwa Watoto (International Day of Play) leo Juni 11, 2025.


 

Post a Comment

Previous Post Next Post