" MWANAMKE MWENYE ULEMAVU MWAJUMA MBOGO AJITOKEZA KUWANIA UDIWANI KATA YA NGOKOLO, BAADA YA KUGUSWA NA HOTUBA YA RAIS SAMIA

MWANAMKE MWENYE ULEMAVU MWAJUMA MBOGO AJITOKEZA KUWANIA UDIWANI KATA YA NGOKOLO, BAADA YA KUGUSWA NA HOTUBA YA RAIS SAMIA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Mwanamke jasiri na mwenye ulemavu, Mwajuma K. Mbogo, leo Juni 29, 2025, ameandika historia mpya kwa kujitokeza kuchukua fomu ya kuwania nafasi ya udiwani katika Kata ya Ngokolo, kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Uamuzi wake umetokana na msukumo alioupata baada ya kusikiliza hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, alipozungumza kwa msisitizo juu ya usawa, ushiriki wa wanawake na watu wenye ulemavu katika uongozi, wakati wa kufunga Bunge la Jamhuri hivi karibuni.

"Hotuba ya Mheshimiwa Rais Samia imenigusa sana. Nimeamua kusimama ili niwe sauti ya walio kimya, hasa wanawake na watu wenye ulemavu. Tunaweza, tukipewa nafasi," amesema Mwajuma mara baada ya kuchukua fomu.

Mwajuma amesema ana uzoefu mkubwa wa kiuongozi, akitaja nyadhifa mbalimbali alizowahi kushika ikiwemo kuwa Mjumbe wa Kamati ya Ustawi wa Jamii, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Tawi la Mwadui mwaka 2015, Mjumbe wa Kamati ya Utekelezaji ya UWT tawi la Mwadui, na kwa sasa ni Mwenyekiti Msaidizi wa Chama cha Watu Wenye Ulemavu wa Viungo Tanzania (CHAWATA) Wilaya ya Shinyanga, sambamba na kuwa Mjumbe wa SHIVYAWATA Wilaya ya Shinyanga Mjini.

Ameeleza kuwa licha ya changamoto alizopitia, ikiwemo kupingwa na baadhi ya watu kwa sababu ya hali yake ya ulemavu wakati wa uchaguzi wa jumuiya ya wazazi, hajawahi kukata tamaa na sasa anaamini ni muda wake wa kusimama kwa ajili ya kuwatumikia wananchi.

"Wakati mwingine unakataliwa si kwa sababu huna uwezo, bali kwa sababu tu ya hali yako. Lakini mimi naamini katika uwezo wa mtu, si kizuizi cha mwili," ameongeza kwa msisitizo.

Zoezi la uchukuaji fomu za kugombea nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya Chama Cha Mapinduzi linaendelea kote nchini, kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

 Mwajuma K. Mbogo, mwanamke jasiri mwenye ulemavu, akipokea fomu ya kuomba ridhaa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kugombea udiwani wa Kata ya Ngokolo, katika ofisi za CCM kata hiyo leo Juni 29, 2025.Mwajuma K. Mbogo

Post a Comment

Previous Post Next Post