" SHINYANGA YAANDIKA HISTORIA: TAMASHA LA UTAMADUNI WA MSUKUMA (SHINYANGA SUKUMA FESTIVAL), LATAMBULIKA MIONGONI MWA MATAMASHA 5 BORA YA KIUTAMADUNI TANZANIA

SHINYANGA YAANDIKA HISTORIA: TAMASHA LA UTAMADUNI WA MSUKUMA (SHINYANGA SUKUMA FESTIVAL), LATAMBULIKA MIONGONI MWA MATAMASHA 5 BORA YA KIUTAMADUNI TANZANIA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Tamasha la Utamaduni wa Msukuma (Shinyanga Sukuma Festival Season 4 ) linalolenga kuenzi na kuendeleza utamaduni wa kabila la Kisukuma linaendelea kufana katika viwanja vya shule ya msingi Nhelegani, Kata ya Kizumbi, Manispaa ya Shinyanga.

Tamasha hilo lililozinduliwa rasmi Julai 18, 2025, linatarajiwa kufikia kilele chake Julai 20, ambapo maelfu ya wakazi wa Mkoa wa Shinyanga na mikoa jirani wameshuhudia michezo ya asili, ngoma za utamaduni, mavazi ya jadi, pamoja na bidhaa mbalimbali zikiuzwa na kuonyeshwa katika mabanda ya maonesho.

Akizungumza wakati wa kuendelea kwa tamasha hilo, muandaaji wake ambaye ni Mkurugenzi wa THE BSL INVESTMENT COMPANY LIMITED AND THE TRUE LIVE FOUNDATION Bwana Peter Frank (MR. BLACK) amesema tamasha hilo lina malengo manne makuu ambayo ni:

1.    Kuendeleza utamaduni wa Msukuma ulioimara, thabiti na makini.

2.    Kutoa fursa kwa wajasiriamali, wafanyabiashara na wadau mbalimbali kutoka Shinyanga na mikoa ya jirani kama Mwanza, Tabora, Geita, Singida na Dodoma kuonyesha huduma na bidhaa zao.

3.    Kuendeleza mshikamano wa kifamilia kwa kukumbuka mila, upendo na urithi kutoka kwa mababu waliotangulia, wakiwemo watawala wa jadi kama mtemi Kudililwa wa Kizumbi.

4.    Kuelimisha na kuhamasisha jamii kushiriki kikamilifu uchaguzi mkuu wa 2025 kwa amani na utulivu chini ya kaulimbiu ya mwaka huu: “Utamaduni wetu, urithi wetu – Shiriki uchaguzi mkuu 2025 kwa amani na utulivu.”

“Tamasha hili limekuwa dira ya maendeleo katika jamii ya Shinyanga. Kwanza limeleta fursa za kiuchumi kupitia mabanda ya maonyesho, pili limefungua milango kwa vijana na vikundi vya asili kuonyesha vipaji na kuhifadhi tamaduni zao, na tatu linaongeza pato la ndani la Manispaa ya Shinyanga kutokana na wageni wengi wanaokuja kushiriki,” amesema Mr. Black.

Mr. Black ameongeza kuwa tamasha hilo limepokelewa vyema na wadau wa utamaduni nchini ambapo limeorodheshwa na Wizara ya Utamaduni kuwa miongoni mwa matamasha matano bora ya utamaduni Tanzania. Pia limetambulika kimataifa kutokana na uwepo wa wageni kutoka mataifa mbalimbali Afrika na nje ya Afrika wanaofuatilia shughuli za tamaduni zinazofanyika kwenye tamasha hilo.

“Tunaomba tamasha hili litambulike rasmi na serikali ya Mkoa wa Shinyanga, kwa heshima ya utawala wa jadi wa mtemi Kidola wa Kizumbi. Litambuliwe kama tamasha la kudumu, lipate vibali na sapoti rasmi ili liweze kukua zaidi na kufikia hadhi ya kitaifa na kimataifa,” amesema Mr. Black.

Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Wilaya ya Shinyanga, Said Kitinga, ambaye alimwakilisha Mkuu wa Wilaya kama mgeni rasmi, amempongeza Mr. Black kwa kuwa kijana mwenye dira, ambaye ameonesha mfano kwa kutumia nguvu zake kuhifadhi na kuendeleza utamaduni wa Mwafrika, hususan wa Wasukuma.

“Kwanza kabisa, ninampongeza Mr. Black kwa moyo wake wa kizalendo na uzalishaji wa fikra chanya kwa jamii. Ametusaidia kutambua utajiri mkubwa uliopo katika utamaduni wetu wa Kisukuma. Kwa niaba ya Serikali, tunathibitisha kuwa tamasha hili linatambulika rasmi na litaendelea kutambulika siku zote,” amesema Kitinga.

Washiriki mbalimbali wa tamasha hilo wametoa pongezi kwa Mr. Black na waandaaji wengine, wakisisitiza umuhimu wa kulifanya tamasha hilo kuwa la kudumu kila mwaka ili kuendeleza urithi wa mababu na kuhamasisha vijana kuenzi mila na desturi zao.

Tamasha la Utamaduni wa Msukuma mkoani Shinyanga lilianzishwa rasmi mwaka 2022 likiwa na kaulimbiu ya kudumu “Lejigukulu lya Nzengo” likimaanisha sherehe au sikukuu ya jamii ya watu wa jadi, na limeendelea kuwa jukwaa muhimu la kutangaza utalii wa kitamaduni, kuunganisha jamii na kuongeza thamani ya urithi wa Kisukuma nchini Tanzania.

Muandaaji wa tamasha hilo ambaye ni Mkurugenzi wa THE BSL INVESTMENT COMPANY LIMITED AND THE TRUE LIVE FOUNDATION Bwana Peter Frank (MR. BLACK) akizungumza.Katibu Tawala wa Wilaya ya Shinyanga, Said Kitinga, akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga.  




Post a Comment

Previous Post Next Post