" TAMASHA LA UTAMADUNI WA MSUKUMA SHINYANGA LAHITIMISHWA KWA NGOMA ZA ASILI, MR. BLACK ASIMIKWA KUWA MSAIDIZI WA CHIFU KIDOLA

TAMASHA LA UTAMADUNI WA MSUKUMA SHINYANGA LAHITIMISHWA KWA NGOMA ZA ASILI, MR. BLACK ASIMIKWA KUWA MSAIDIZI WA CHIFU KIDOLA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Tamasha la Shinyanga Sukuma Festival Season 4 limehitimishwa Julai 20, 2025 kwa shamrashamra za michezo ya asili, burudani ya ngoma za jadi na ushiriki mkubwa wa wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Shinyanga na mikoa jirani.

Akifunga tamasha hilo kwa heshima na mila za jadi, Mgeni rasmi ambaye ni Mwenyekiti wa Machifu Mkoa wa Shinyanga, Chifu Kidola Njange, ametangaza rasmi kumsimika Mr. Black kuwa msaidizi wake wa heshima, ndani ya himaya ya utemi wa Kizumbi, ikiwa ni kutambua mchango wake mkubwa wa kulinda, kukuza na kuendeleza utamaduni wa Kisukuma.

Katika hotuba yake, Chifu Kidola amewaasa wananchi kuendelea kuenzi mila na desturi njema zilizoasisiwa na watemi waliotangulia, akisema utamaduni ni nguzo ya taifa na sehemu ya amani.

“Tuendelee kuitunza amani ya nchi yetu kupitia mila zetu. Tuishi kwa mshikamano, upendo na heshima kama tulivyolelewa na mababu zetu. Mwaka huu tunakwenda kwenye uchaguzi mkuu, nawaomba mshiriki kwa amani, mchangie viongozi bora watakaolinda utu, maendeleo na mila zetu,” amesema Chifu Kidola.

Kwa upande wake, Mr. Black ambaye ndiye muasisi na muandaaji mkuu wa tamasha hilo, ameushukuru uongozi wa jadi kwa heshima hiyo kubwa, na kueleza kuwa tamasha hilo ni endelevu na litazidi kuwa kubwa kila mwaka.

Ameeleza kuwa kuanzia mwakani 2026, tamasha hilo litabadilika jina na kuitwa rasmi "SHINYANGA KIZUMBI SUKUMA FESTIVAL", ili kuipa heshima ya kudumu historia ya utemi wa Kizumbi na mizizi ya utamaduni wa Wasukuma.

“Ninawashukuru sana wananchi, wafanyabiashara, viongozi wa serikali, machifu, vikundi vya utamaduni, taasisi na kila mmoja aliyeshiriki kwa namna yoyote. Tumeandika historia ya utamaduni wetu – historia ambayo haifutiki,” amesema Mr. Black.

Katika uwanja wa shule ya msingi Nhelegani, ambapo tamasha hilo limefanyika kwa siku tatu mfululizo, maelfu ya wananchi walijitokeza kushuhudia ngoma za jadi, maigizo ya asili, mavazi ya kitamaduni, pamoja na mabanda ya maonyesho ya bidhaa na huduma kutoka kwa wafanyabiashara wa ndani.

Washiriki wengi wameomba tamasha hilo liwe la kudumu na lijumuishwe rasmi katika kalenda ya matukio ya utamaduni ya taifa, wakisema linaongeza mshikamano wa kijamii, kukuza uchumi na kutangaza utambulisho wa Mtanzania kwa mataifa ya nje.

Tamasha la Sukuma Festival lilianzishwa mwaka 2022 chini ya kaulimbiu ya “Lejigukulu vya Nzengo” likiwa na dhamira ya kulinda urithi wa Kisukuma, na mwaka huu limeorodheshwa rasmi kuwa miongoni mwa matamasha matano bora ya kiutamaduni nchini Tanzania kwa mujibu wa Wizara ya Utamaduni.


 

Post a Comment

Previous Post Next Post