" HALMASHAURI YA WILAYA GEITA YAVUKA LENGO LA MAPATO KWA ASILIMIA 125.19

HALMASHAURI YA WILAYA GEITA YAVUKA LENGO LA MAPATO KWA ASILIMIA 125.19


 

 

Ukusanyaji wa mapato umeendelea kuwa ajenda ya kudumu katika vikao vya Timu ya Menejimenti ya Halmashauri ya Wilaya ya Geita, ikiwa ni moja ya nguzo muhimu ya utekelezaji wa shughuli za maendeleo.

 

Katika mwaka wa fedha 2024/2025, Halmashauri hiyo imevunja rekodi kwa kuvuka lengo la ukusanyaji wa mapato kwa asilimia 125.19. Jumla ya shilingi bilioni 10.4 zimekusanywa, ikiwa ni ongezeko la shilingi bilioni 2.1 kutoka kwenye bajeti iliyokasimiwa ya shilingi bilioni 8.3.

 

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Ndg. Karia Rajab Magaro, amewasihi watendaji wote wa Halmashauri kuendelea kuwa waadilifu na wabunifu katika usimamizi wa mapato, huku akisisitiza kudhibiti mianya ya upotevu wa fedha ili kuongeza ufanisi wa kiutendaji.

 

Kupitia usimamizi bora wa mapato ya ndani, miradi mbalimbali ya maendeleo imetekelezwa kwa mafanikio makubwa. Kwa mwaka wa fedha 2024/2025, kiasi cha shilingi bilioni 3.1 kimetengwa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi inayojumuisha ujenzi wa shule, zahanati, vituo vya afya, nyumba za watumishi na ofisi za kata.

 

Aidha, kupitia mapato ya ndani na fedha za marejesho, Halmashauri imefanikiwa kutoa mikopo ya asilimia 10 kwa makundi maalum ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Jumla ya shilingi bilioni 1.8 zimelipwa kwa wananchi waliokidhi vigezo vya kupokea mikopo hiyo.

 

Katika kuimarisha zaidi huduma kwa wananchi, Halmashauri imeendelea na mkakati wa kutwaa maeneo ya uwekezaji, ikiwa ni hatua ya kuongeza vyanzo vya mapato na kuendeleza miundombinu ya kijamii na kiuchumi.

 

Mnamo Julai 24, 2025, Timu ya Menejimenti ya Halmashauri ya Wilaya ya Geita ikiongozwa na Kaimu Mkurugenzi, CPA Eveline Ntahamba, ilifanya ziara katika Mamlaka ya Mji Mdogo wa Katoro kwa lengo la kukagua maeneo ya uwekezaji. Ziara hiyo ilihusisha eneo lenye ukubwa wa hekari 14 linalotarajiwa kutwaliwa kwa ajili ya ujenzi wa stendi ya mabasi (Katoro Bus Stand) pamoja na soko la Kariakoo Katoro.

 

Kwa hatua hizo, Halmashauri ya Wilaya ya Geita inaendelea kuishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mchango mkubwa wa fedha katika kufanikisha shughuli mbalimbali za maendeleo.

 


Post a Comment

Previous Post Next Post