" MWENGE WA UHURU 2025 WARIDHISHWA NA MIRADI YOTE 8 YA MAENDELEO HALMASHAURI YA WILAYA YA SHINYANGA, WANANCHI WAASWA KUSHIRIKI UCHAGUZI MKUU 2025

MWENGE WA UHURU 2025 WARIDHISHWA NA MIRADI YOTE 8 YA MAENDELEO HALMASHAURI YA WILAYA YA SHINYANGA, WANANCHI WAASWA KUSHIRIKI UCHAGUZI MKUU 2025

Na Mapuli Kitina Misalaba

Mwenge wa Uhuru 2025 umeendelea na mbio zake ambapo leo Agosti 6, 2025 umekimbizwa kwa jumla ya kilomita 258.5 na kumulika miradi mbalimbali ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya Shilingi Bilioni 2.8 katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.

Kwa kauli mbiu isemayo "Jitokeze Kushiriki Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 kwa Amani na Utulivu", Mwenge wa Uhuru umefungua, kuzindua, kukagua na kuweka mawe ya msingi kwenye jumla ya miradi 8 inayolenga kuboresha maisha ya wananchi.

Akizungumza wakati wa mapokezi ya mwenge huo katika eneo la, Kigwang'ona, kata ya Puni kabla ya kuanza mbio hizo, Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Wakili Julius Mtatiro, amesema kuwa Mwenge huo utakagua miradi 4, utafungua miradi 3, utazindua miradi 4 na kuweka mawe ya msingi kwenye miradi 6, ukiwa ni sehemu ya kuchochea maendeleo ya wananchi.

Miradi iliyomulikwa ni pamoja na:

1.    Kituo cha Mafunzo ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi Kata ya Didia – kilichopo katika ofisi ya maafisa ugani, mradi huu unalenga kutoa elimu ya vitendo kwa wakulima na wafugaji.

2.    Mradi wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia – uliozinduliwa katika Shule ya Awali na Msingi Ola kwa lengo la kulinda afya za walimu na wanafunzi dhidi ya moshi hatarishi.

3.    Klabu ya Wapinga Rushwa – imezinduliwa katika Shule ya Sekondari Ilola ili kuimarisha maadili na kupambana na vitendo vya rushwa miongoni mwa wanafunzi.

4.    Uwezeshaji wa Vijana Kiuchumi – kupitia Kikundi cha Amani Ihalo ambapo vijana wamewezeshwa kupitia mkopo wa asilimia 10 kutoka mapato ya Halmashauri.

5.    Mradi wa Maji Kijiji cha Mwamakalanga, Kata ya Lyabukande – umetembelewa, kukaguliwa na kuwekwa jiwe la msingi ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama.

6.    Kituo cha Afya Lyabukande – mwenge wa uhuru umeweka jiwe la msingi katika kituo hiki chenye umuhimu mkubwa katika utoaji wa huduma za afya vijijini.

7.    Ujenzi wa Machinjio Ndogo ya Mifugo Kata ya Solwa – mradi huu unalenga kuboresha usafi, afya na uchumi kupitia sekta ya mifugo.

8.    Shule ya Amali Mwambasha – inajengwa kwa ajili ya kuwapatia vijana elimu ya ufundi na kuwawezesha kujiajiri.

Kwa upande wake, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025, Ismail Ali Ussi, amesema ameridhishwa na ubora wa utekelezaji wa miradi hiyo na kupongeza uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, hususan Mkurugenzi Dkt. Kalekwa Kasanga kwa usimamizi makini na ubunifu mkubwa.

Ussi ameongeza kuwa miradi hiyo inaonesha dhamira ya dhati ya serikali ya kuwaletea wananchi maendeleo, huku akiwasisitiza wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki uchaguzi mkuu 2025 kwa amani, utulivu na mshikamano.

"Rais Samia Suluhu Hassan amefanya mambo makubwa katika muda mfupi. Ni kiongozi wa mfano na wananchi wanapaswa kuendelea kumwamini kwa ajili ya mustakabali wa taifa letu," amesema Ussi.

Mwenge wa Uhuru unaendelea na mbio zake mkoani Shinyanga ambapo kesho Agosti 7, 2025 unatarajiwa kukimbizwa katika Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, ukiendelea kuhamasisha amani, mshikamano, mapambano dhidi ya rushwa na ushiriki wa wananchi katika maendeleo ya taifa.

PICHA ZITAENDELEA

 

Post a Comment

Previous Post Next Post