" WAENDESHA BAJAJI SHINYANGA WAPEWA ELIMU YA KUPISHA MAGARI YALIYOBEBA WAGONJWA BARABARANI

WAENDESHA BAJAJI SHINYANGA WAPEWA ELIMU YA KUPISHA MAGARI YALIYOBEBA WAGONJWA BARABARANI

Madereva wa Bajaji katika Manispaa ya Shinyanga wamepatiwa elimu maalum ya umuhimu wa kutoa kipaumbele kwa magari yanayobeba wagonjwa yanapokuwa yakipita barabarani, ili kuhakikisha huduma za dharura zinawafikia wagonjwa kwa wakati.

Elimu hiyo imetolewa Askari Polisi wa kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Shinyanga Sajenti David Ndimila, ambaye amewaasa waendesha bajaji kutochukulia ving’ora vya magari ya wagonjwa kama kelele za kawaida, bali kama ishara ya dharura inayohitaji msaada wa haraka.

Sajenti Ndimila amesema kuwa kuchelewesha magari ya wagonjwa kwa kuyazuia barabarani kunaweza kuhatarisha maisha ya watu, hivyo ni wajibu wa kila dereva kuhakikisha anapisha njia mara tu anaposikia ving’ora.

“Tunawaomba sana madereva wa bajaji na vyombo vingine vya usafiri kuwa na uelewa mkubwa. Magari haya ya wagonjwa mara nyingi hubeba watu walioko kwenye hali mbaya. Kila sekunde ni muhimu katika kuokoa maisha yao. Tukiwapisha mapema, tunasaidia kuokoa maisha,” amesema Sajenti Ndimila.

Aidha, amewataka madereva hao kufuata sheria na alama za barabarani, huku akisisitiza mshikamano na ushirikiano kati yao na askari wa usalama barabarani ili kupunguza ajali na kurahisisha utendaji kazi wa vyombo vya dharura.

Madereva wa bajaji waliopatiwa elimu hiyo wameshukuru kwa mafunzo hayo na kuahidi kuyafanyia kazi, huku wakitoa wito kwa madereva wenzao wote kuhakikisha wanafuata maagizo ya usalama barabarani kwa manufaa ya jamii.


 

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

Post a Comment

Previous Post Next Post