" PROF. SHEMDOE AWAELEKEZA WALIMU WAKUU KUDHIBITI UTORO WA WANAFUNZI NA WALIMU SHULENI

PROF. SHEMDOE AWAELEKEZA WALIMU WAKUU KUDHIBITI UTORO WA WANAFUNZI NA WALIMU SHULENI






Waziri wa Nchi, Ofisi wa Waziri Mkuu – TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe akiwaelekeza Walimu Wakuu wa Shule za Sekondari (hawapo pichani) kudhibiti utoro wa wanafunzi na walimu shuleni, wakati akifungua Mkutano wa 20 wa Wakuu wa Shule za Sekondari Tanzania (TAHOSSA), uliofanyika Jijini Arusha katika Ukumbi wa Tanzania Convention Center (Ngurudoto).

Baadhi ya Walimu Wakuu wa Shule za Sekondari wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi wa Waziri Mkuu – TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe (hayupo pichani), wakati akifungua Mkutano wa 20 wa Wakuu wa Shule za Sekondari Tanzania (TAHOSSA), uliofanyika Jijini Arusha katika Ukumbi wa Tanzania Convention Center (Ngurudoto).

Waziri wa Nchi, Ofisi wa Waziri Mkuu – TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe akiwa na baadhi ya viongozi, akielekea kuingia katika Ukumbi wa Tanzania Convention Center (Ngurudoto) kwa ajili ya kufungua Mkutano wa 20 wa Wakuu wa Shule za Sekondari Tanzania (TAHOSSA) uliofanyika katika ukumbi huo uliopo jijini Arusha.



Waziri wa Nchi, Ofisi wa Waziri Mkuu – TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe akisalimiana na baadhi ya viongozi waliompokea, mara baada ya kuwasili katika Ukumbi wa Tanzania Convention Center (Ngurudoto) kwa ajili ya kufungua Mkutano wa 20 wa Wakuu wa Shule za Sekondari Tanzania (TAHOSSA), uliofanyika kwenye ukumbi huo uliopo jijini Arusha.

…………..

Na James K. Mwanamyoto

Waziri wa Nchi, Ofisi wa Waziri Mkuu – TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewaelekeza Walimu Wakuu wa Shule za Sekondari na Msingi nchini kuhakikisha wanadhibiti changamoto ya utoro kwa wanafunzi na walimu katika shule wanazozisimamia.

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo, wakati akifungua Mkutano wa 20 wa Wakuu wa Shule za Sekondari Tanzania (TAHOSSA), uliofanyika Jijini Arusha katika Ukumbi wa Tanzania Convention Center (Ngurudoto Mountain Lodge).

“Walimu Wakuu nendeni mkadhibiti utoro wa wanafunzi na walimu shuleni, wapo baadhi ya walimu wakiripoti kazini asubuhi baada ya muda mfupi wanaenda kufanya kazi ya bodaboda mtaani,” Prof. Shemdoe amesisitiza.

Prof. Shemdoe amefafanua kuwa, Walimu Wakuu wakidhibiti utoro shuleni watakuwa wamelihakikishia taifa kupata wanafunzi wenye ufaulu mzuri, nidhamu bora, ujuzi wa maisha na moyo wa kizalendo.

Ameongeza kuwa, utoro unasababisha anguko la kitaaluma katika taifa, hivyo Walimu Wakuu wanapaswa kudhibiti utoro wa wanafunzi na walimu ili kutengeneza rafiki ya kuinua kiwango cha taaluma nchini, ikiwa ni pamoja na kuwawezesha vijana kufikia ndoto zao.

Akizungumzia suala la walimu kuwa na vyanzo mbadala vya kuongeza kipato, Prof. Shemdoe amesema kwamba Serikali haikatazi watumishi kuwa na shughuli mbadala za kuwaongezea kipato, iwapo shughuli hizo zitafanywa na watumishi mara baada ya muda wa kazi wa Serikali.

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amewataka Wakuu wa Shule kuwa chachu ya kuwapatia watanzania tabasamu la kweli kwa kudhibiti utoro wa wanafunzi na walimu, ambao kitaaluma ni kikwazo cha wanafunzi kupata ufaulu mzuri.

Kwa maelekezo haya, Prof. Riziki Shemdoe ameunga mkono kwa vitendo jitihada za Serikali za kuendelea kuchukua hatua madhubuti ya kuimarisha nidhamu, uwajibikaji na ubora wa elimu nchini.

Post a Comment

Previous Post Next Post