Katibu wa Jumuiya ya Wazazi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Mpanda, Ndugu Jimotoli Jilala Maduka, katikati akipanda mti.
Katibu wa Jumuiya ya Wazazi wa Chama Cha Mapinduzi
(CCM) Wilaya ya Mpanda, Ndugu Jimotoli
Jilala Maduka, leo tarehe 28 Januari 2026 ameshiriki kikamilifu zoezi la
upandaji wa miti lililofanyika katika Kata ya Shanwe, Manispaa ya Mpanda, Mkoa
wa Katavi, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu
Hassan, katika kulinda mazingira.
Ndugu Maduka ameshiriki zoezi hilo kwa niaba ya Katibu
wa CCM Wilaya ya Mpanda, Ndugu Musa Ramadhan
Mwevi, katika zoezi lililoongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Bi. Mwamvua Mrindoko, likihusisha
viongozi wa Serikali, Chama na wananchi wa Mkoa wa Katavi.
Katika zoezi hilo, Ndugu Jimotoli Jilala Maduka ameonesha mshikamano na uzalendo kwa
kushiriki moja kwa moja upandaji wa miti, akieleza kuwa Jumuiya ya Wazazi CCM
itaendelea kuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha jamii kushiriki kikamilifu
katika utunzaji wa mazingira kama sehemu ya wajibu wa kizalendo na maendeleo
endelevu ya Taifa.
Ndugu Maduka amesisitiza kuwa upandaji wa miti ni
ajenda ya kudumu inayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja, hivyo Jumuiya ya
Wazazi CCM Wilaya ya Mpanda itaendelea kushirikiana na Serikali na wananchi
katika kuhamasisha upandaji miti kuanzia ngazi ya familia hadi jamii kwa
ujumla.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Mkuu wa Mkoa wa
Katavi, Bi. Mwamvua Mrindoko,
amewahamasisha wananchi wa Kata ya Shanwe, Manispaa ya Mpanda na Mkoa wa Katavi
kwa ujumla kupanda miti katika kila mtaa ili kuboresha na kutunza mazingira ya
maeneo wanayoishi.
Amesisitiza umuhimu wa upandaji miti katika maeneo
muhimu yakiwemo ofisi za kazi, shule, hospitali, barabara, makazi ya wananchi
pamoja na maeneo mengine ya kijamii.
Bi. Mrindoko ameeleza kuwa kila mtaa na kila kaya
inapaswa kupanda angalau miche mitatu au zaidi kama mfano wa kuigwa katika
jamii, hatua itakayosaidia kuleta muonekano mzuri wa mazingira na kuimarisha
utunzaji wa rasilimali asilia katika Mkoa wa Katavi.
Katika hatua nyingine, Mkuu wa Mkoa wa Katavi
amewahamasisha wananchi kuwa mabalozi wazuri wa elimu kwa kuhakikisha watoto
wanapelekwa shule kuendelea na masomo ya elimu ya msingi na sekondari,
akisisitiza kuwa kila mwananchi ana wajibu wa kuhamasisha zoezi hilo nyumba kwa
nyumba.
Akizungumzia suala la elimu, Ndugu Jimotoli Jilala Maduka ameungana na Mkuu wa Mkoa kwa
kusisitiza umuhimu wa Jumuiya ya Wazazi CCM kushiriki kikamilifu katika
kuhimiza mahudhurio ya wanafunzi shuleni, akieleza kuwa elimu ni msingi wa
maendeleo ya familia na Taifa kwa ujumla.
Aidha, Bi. Mrindoko amewahimiza wananchi kushiriki
zoezi la upandaji miti kila tarehe 27 ya kila mwezi katika wilaya zote za Mkoa
wa Katavi, kama sehemu ya kuunga mkono juhudi za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kulinda mazingira na kukabiliana
na athari za mabadiliko ya tabia ya nchi.
Naye Ndugu
Jimotoli Jilala Maduka ameeleza kuwa Jumuiya ya Wazazi CCM Wilaya ya
Mpanda itaendelea kuhamasisha wanachama na wananchi kushiriki zoezi hilo la
kila mwezi, akibainisha kuwa upandaji miti ni urithi muhimu kwa vizazi vijavyo.
Zoezi hilo pia limeshuhudiwa na Mkuu wa Wilaya ya
Mpanda, Bi. Jamila Yusuph,
ambaye ameshiriki kupanda miti pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Katavi kama ishara ya
umoja na mshikamano wa viongozi katika kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania.
Mkuu wa Wilaya ametumia fursa hiyo kuwakumbusha
wananchi wa Wilaya ya Mpanda umuhimu wa kuwapeleka watoto shule na kuwa
mabalozi wa elimu katika jamii.
Zoezi la upandaji miti limeelezwa kuwa ni hatua muhimu
ya kuimarisha utunzaji wa mazingira, kuendeleza rasilimali asilia na kuimarisha
umoja na ushirikiano wa jamii katika Mkoa wa Katavi.
Aidha, zoezi hilo limefanyika sambamba na kumbukizi ya
siku ya kuzaliwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambapo
limechukuliwa kama ishara ya heshima, uzalendo, mshikamano na upendo kwa
kiongozi mkuu wa nchi.
Kauli mbiu ya zoezi hilo ilikuwa:
“UZALENDO NI KUTUNZA MAZINGIRA, SHIRIKI
KUPANDA MITI.”
Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Bi. Mwamvua Mrindoko, akizungumza kwenye zoezi hilo la upandaji miti.
Mkuu wa Wilaya ya Mpanda, Bi. Jamila Yusuph, akizungumza.




Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Bi. Mwamvua Mrindoko, akikabidhi miti kwa wananchi.
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254










Post a Comment