" SHY TALENT FILMS YAANZA MAZOEZI, VIONGOZI WAWATIA MOYO VIJANA KUPAMBANIA VIPAJI VYAO

SHY TALENT FILMS YAANZA MAZOEZI, VIONGOZI WAWATIA MOYO VIJANA KUPAMBANIA VIPAJI VYAO


Baadhi ya wanakikundi cha SHY TALENT FILMS leo Jumatano Januari 14, 2026 wameanza rasmi mazoezi ya awali, hatua inayochukuliwa kama mwanzo wa safari ya kutumia sanaa kuelimisha jamii na kuibua vipaji vya vijana katika Manispaa ya Shinyanga.

Mgeni rasmi katika mazoezi hayo ni Mwenyekiti wa Wenyeviti wa Mitaa Manispaa ya Shinyanga ambaye pia ni Mwenyekiti wa Mtaa wa Miti Mirefu, Bwana Nassor Mokhe Warioba, sambamba na Mtendaji wa Mtaa wa Miti Mirefu Amgelight Emmanuel Mwanri, ambao wamepata nafasi ya kuzungumza na vijana hao na kuwatia moyo.

Akizungumza katika mazoezi hayo, Bwana Nassor Warioba amewahimiza vijana kutokukata tamaa katika kupambania vipaji vyao, akisisitiza kuwa safari ya mafanikio katika sanaa inahitaji uvumilivu, nidhamu na kujitambua huku akisema vipaji vingi vimekufa si kwa kukosa uwezo, bali kwa wahusika kukosa msaada wa kisaikolojia na uongozi unaoeleweka.

Ameipongeza Taasisi ya Misalaba Media kwa kuanzisha kikundi cha SHY TALENT FILMS, akisema ni wazo lenye tija kubwa kwa jamii na litakalosaidia kufungua fursa za ajira na kujiajiri kwa wananchi wa Manispaa ya Shinyanga, hususan vijana wenye vipaji vya sanaa.

Bwana Mokhe amesema kwa muda mrefu vipaji vingi vimekuwa vikikosa mwelekeo kutokana na ukosefu wa majukwaa ya kuwaendeleza vijana, hivyo kuanzishwa kwa SHY TALENT FILMS ni hatua muhimu ya kutumia sanaa kama nyenzo ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Ameongeza kuwa viongozi wa mitaa wako tayari kushirikiana na kikundi hicho katika kuhakikisha vipaji vinatambuliwa na kulindwa.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Mtaa wa Miti Mirefu, Amgelight Emmanuel Mwanri, amewapongeza vijana kwa uamuzi wao wa kujiunga na kikundi chenye mwelekeo wa kuelimisha jamii, akiwataka kuitumia sanaa kama sauti ya mabadiliko chanya, hususan katika masuala yanayogusa maisha ya kila siku ya jamii.

Katika hatua nyingine, Bwana Nassor Warioba amependekezwa kuwa miongoni mwa walezi wa kikundi cha SHY TALENT FILMS, pendekezo alilolipokea na kuahidi kuwa mshauri mzuri kwa vijana hao, akiahidi kushirikiana nao katika kuwajenga kimaadili, kiakili na kijamii.

Mkurugenzi wa Misalaba Media, Mapuli Misalaba, amewashukuru viongozi hao kwa kukubali kushiriki katika mazoezi ya awali ya kikundi hicho, akisema ushiriki wao ni chachu ya kuwajengea vijana imani, morali na mwelekeo sahihi wa safari ya sanaa.

Kwa upande wake Meneja wa Misalaba Media ambaye pia ni Katibu wa SHY TALENT FILMS, Daniel Sibu, ameeleza kuwa kikundi hicho kimejipanga kufanya kazi kwa nidhamu, uwazi na malengo yaliyo wazi, huku akisisitiza kuwa SHY TALENT FILMS si kikundi cha burudani pekee bali ni darasa la maisha kwa vijana.

Naye Mwenyekiti wa SHY TALENT FILMS, Daniel Elimboto, amewashukuru viongozi wa serikali ya mtaa na manispaa kwa moyo wao wa kuunga mkono vijana, akisema ahadi waliyoitoa ya kuwa karibu na kikundi hicho itasaidia kukilea na kukijenga katika misingi ya uwajibikaji na weledi.

Mazoezi hayo yameanza kwa mtindo wa kipekee kwa kusikiliza, kufikiri, kuhoji na kujifunza kwa njia shirikishi inayogusa maisha halisi ya jamii ambapo kabla ya kuanza kuandika script, washiriki wameanza kwa maswali; kabla ya kuigiza, wameanza kwa uelewa.

Kila mshiriki amekuwa sehemu ya darasa la maisha, akitafakari nguvu ya maneno, maamuzi na mchango wa kila mmoja katika kujenga au kubomoa ndoto za wengine.

SHY TALENT FILMS ni kikundi cha sanaa kilichoanzishwa na Misalaba Media, chombo cha habari cha mtandaoni kilichosajiliwa kisheria, kinachojishughulisha na ukusanyaji, uchakataji na usambazaji wa habari, huku kikitumia pia sanaa na ubunifu kama nyenzo ya kuelimisha, kuhamasisha na kuijenga jamii.

Kwa taarifa zaidi kuhusu shughuli za kikundi hiki, tembelea ukurasa wao mpya wa Instagram unaoitwa SHY TALENT FILMS.

“Kuibua vipaji leo, Kujenga wasanii wa kesho.”

Mgeni rasmi katika mazoezi hayo ni Mwenyekiti wa Wenyeviti wa Mitaa Manispaa ya Shinyanga ambaye pia ni Mwenyekiti wa Mtaa wa Miti Mirefu, Bwana Nassor Mokhe Warioba, akizungumza kwenye mazoezi hayo.

Mgeni rasmi katika mazoezi hayo ni Mwenyekiti wa Wenyeviti wa Mitaa Manispaa ya Shinyanga ambaye pia ni Mwenyekiti wa Mtaa wa Miti Mirefu, Bwana Nassor Mokhe Warioba, akizungumza kwenye mazoezi hayo.

Mkurugenzi wa Misalaba Media, Mapuli Misalaba, akimshukuru Mwenyekiti wa Wenyeviti wa Mitaa Manispaa ya Shinyanga ambaye pia ni Mwenyekiti wa Mtaa wa Miti Mirefu, Bwana Nassor Mokhe Warioba, kwa kuwasili katika mazoezi hayo.

Mtendaji wa Mtaa wa Miti Mirefu, Amgelight Emmanuel Mwanri, akiwapongeza vijana kwa uamuzi wao wa kujiunga na kikundi hicho.

Meneja wa Misalaba Media ambaye pia ni Katibu wa SHY TALENT FILMS, Daniel Sibu, akizungumza kwenye mazoezi hayo.

Mwenyekiti wa SHY TALENT FILMS, Daniel Elimboto, akiwashukuru viongozi wa serikali ya mtaa na manispaa kwa moyo wao wa kuunga mkono vijana.





Picha ya pamoja.

 

Post a Comment

Previous Post Next Post