" WANANCHI SHINYANGA WAWAHIMIZA WATANZANIA KUENDELEA KUYAENZI MAZURI YA HAYATI DKT. JOHN POMBE MAGUFULI

WANANCHI SHINYANGA WAWAHIMIZA WATANZANIA KUENDELEA KUYAENZI MAZURI YA HAYATI DKT. JOHN POMBE MAGUFULI


Na Edington Mukiza Ezron, Misalaba Media

Wananchi mkoani Shinyanga wameungana na Watanzania wengine kuadhimisha kumbukizi ya miaka mitano ya kifo cha aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli, kwa kukumbuka na kuthamini mchango wake katika maendeleo ya taifa.

Baadhi ya wananchi katika Manispaa ya Shinyanga, wakizungumza na Misalaba Media leo Machi 17, 2026, wamesema hayati Magufuli ataendelea kukumbukwa kwa uadilifu wake, uchapakazi pamoja na msimamo wake thabiti katika kusimamia rasilimali za nchi.

Mmoja wa wananchi hao, Daud Peter Philipo, amesema kuwa kuna mambo mengi mazuri aliyoyaacha hayati Magufuli ambayo yanapaswa kuenziwa na kizazi cha sasa na kijacho.

Ameeleza kuwa kiongozi huyo aliweka kipaumbele katika uwajibikaji na nidhamu ya kazi, hali iliyochochea maendeleo ya uchumi na kuongeza imani ya wananchi kwa serikali yao.

“Watanzania hatuna budi kuyaenzi mema yote aliyoyafanya, kwani yamechangia kwa kiasi kikubwa kukuza uchumi na kuimarisha ustawi wa taifa kwa ujumla,” amesema Philipo.

Kwa upande wake, mjasiriamali Steward Mathias amesema anatamani kuona serikali ya sasa ikiendeleza yale yote mazuri yaliyoanzishwa na hayati Magufuli, hususan katika kusikiliza kero za wananchi wa kada zote, jambo alilodai kuwa ni msingi muhimu wa utawala bora na demokrasia.

Mathias ameongeza kuwa katika kipindi cha uongozi wa hayati Magufuli, Tanzania ilipiga hatua kubwa katika sekta ya miundombinu, ikiwemo ujenzi wa barabara za kisasa na madaraja ya juu (flyovers) yaliyosaidia kupunguza msongamano wa magari mijini, sambamba na kuboreshwa kwa huduma za kijamii kama maji, umeme na elimu.

Aidha, wananchi hao wamekumbusha umuhimu wa kuenzi misingi ya maadili aliyokuwa akiisisitiza hayati Magufuli, ikiwemo kuwa na imani, hofu ya Mungu na uzalendo, wakieleza kuwa hayo ni nguzo muhimu katika kujenga jamii imara na yenye maendeleo.

Maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka mitano ya kifo cha hayati Magufuli yamefanyika kitaifa nyumbani kwake kwa hayati Magufuli Chato mkoani Geita, ambapo viongozi mbalimbali na wananchi wameshiriki ibada maalum ya kumuombea pamoja na kutembelea kaburi lake, ikiwa ni ishara ya heshima na kuthamini mchango wake kwa taifa.

   

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment

Previous Post Next Post