Askofu wa Jimbo Katoliki la Shinyanga, Mhashamu Liberatus Sangu, amepokea miche 100 ya miti ya matunda, mbao na kivuli kutoka taasisi ya Joseph Muhunda Nyerere Foundation kwa lengo la kuendeleza juhudi za utunzaji wa mazingira
Akizungumza katika hafla ya makabidhiano ya miche hiyo, Askofu Sangu amepongeza hatua hiyo na kusema kuwa ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za kitaifa za kuhifadhi mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Amepongeza hatua hiyo na kubainisha kuwa utunzaji wa mazingira ni wajibu wa kila mmoja, na kwamba ni hatua nyingine katika kuunga mkono juhudi za Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, za kuhimiza uhifadhi wa mazingira nchini.
Aidha, Askofu Sangu amesema kuwa juhudi hizo zinaendana na mafundisho ya hayati Baba Mtakatifu Fransisko, ambaye enzi za uhai wake alikuwa akisisitiza umuhimu wa kulinda mazingira kama sehemu ya kushiriki katika uumbaji wa Mungu
Amesema pamoja na kulinda mazingira, ni muhimu pia taasisi hiyo ikajikita katika juhudi za kudumisha amani, kuipenda nchi yao na kuwa wazalendo wa kweli.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Taasisi hiyo Joseph Muhunda Nyerere amesema amepokea maelekezo hayo na kuahidi kuyazingatia. ameeleza kuwa ataendelea kuhamasisha jamii kuishi kwa kuzingatia misingi ya amani, uzalendo na uwajibikaji sambamba na kuendeleza kampeni za uhifadhi wa mazingira nchini.
Taasisi ya JOSEPH MUHUNDA NYERERE FOUNDATION inajihusisha na masuala ya uhifadhi wa mazingira Nchini.









Post a Comment