" MARY MAKAMBA ATUMIA SIKU YA WAPENDANAO KUSAIDIA WAGONJWA KWA KUGAWA MASHUKA 60 ZAHANATI YA ADVENT HEALTH CARE BUGWETO A

MARY MAKAMBA ATUMIA SIKU YA WAPENDANAO KUSAIDIA WAGONJWA KWA KUGAWA MASHUKA 60 ZAHANATI YA ADVENT HEALTH CARE BUGWETO A

Na Mapuli Kitina Misalaba

Katika kuadhimisha Siku ya Wapendanao, Mwenyekiti wa Mtaa wa Bugweto A, Mary Makamba, ameambatana na wajumbe wa Serikali ya Mtaa huo na kukabidhi msaada wa mashuka 60 kwa ajili ya wagonjwa katika Advent Health Care Dispensary iliyopo Manispaa ya Shinyanga.

Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, Bi. Mary Makamba amesema ameamua kuitumia siku hiyo maalum ya wapendanao kwa kusaidia kutatua changamoto za kijamii ndani ya mtaa wake, badala ya kuisherehekea kwa namna ya kawaida.

Amesema zahanati hiyo ndiyo kituo kinachowahudumia wananchi wa Bugweto A wanapokumbwa na changamoto za kiafya, wakifika kwa ajili ya uchunguzi na matibabu ya awali, hivyo ni muhimu jamii kuendelea kuiunga mkono ili iweze kutoa huduma bora zaidi.

Ametoa wito kwa wananchi na viongozi wengine kuiga mfano huo kwa kuwakumbuka watu wenye uhitaji, hasa wagonjwa na makundi maalum, ili kuifanya Siku ya Wapendanao kuwa na maana pana zaidi ya kijamii.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa zahanati hiyo ambaye pia ni Mratibu wa Magonjwa Yasiyo ya Kuambukiza Manispaa ya Shinyanga, Dkt. Lameck Mihayo, ameishukuru Serikali ya Mtaa wa Bugweto A kwa msaada huo akisema utasaidia kupunguza changamoto zilizokuwa zinajitokeza hususan pale kunapokuwa na wagonjwa wengi wanaohitaji huduma kwa wakati mmoja.

Amesema mashuka hayo yatasaidia kuboresha mazingira ya huduma kwa wagonjwa na kuongeza faraja wanapokuwa wanapatiwa matibabu.

Bi. Mary Makamba (wa pili kutoka kushoto), Mwenyekiti wa Mtaa wa Bugweto A, akikabidhi mashuka kwa madaktari wa Advent Health Care Dispensary ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha Siku ya Wapendanao.

 

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment

Previous Post Next Post