Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James, amefungua rasmi
kongamano la wadau wa habari lililoandaliwa na Taasisi ya Vyombo vya Habari
Kusini mwa Jangwa la Sahara,Tawi la Tanzania (MISA TAN) mkoani humo, huku
akiipongeza taasisi hiyo kwa kuendelea kusimamia weledi na maendeleo ya sekta
ya habari nchini.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kongamano hilo,
James amesema ameridhishwa na maono ya MISA Tanzania katika kuimarisha uhuru wa
vyombo vya habari pamoja na kukuza mchango wa sekta hiyo katika maendeleo ya
jamii.
Amesema Mkoa wa Iringa unaendelea kukua kiuchumi
kutokana na shughuli mbalimbali za maendeleo ikiwemo kilimo, biashara, elimu na
uwekezaji wa viwanda, huku akitaja mazao kama mahindi na maharage kuwa miongoni
mwa mazao muhimu yanayochangia uchumi wa mkoa huo.
James ameeleza kuwa Iringa pia ina vivutio mbalimbali
vya utalii kama Bwawa la Mtela, Hifadhi ya Taifa ya Ruaha pamoja na maeneo ya
kihistoria kama historia ya Mtemi Mbwao, ambavyo vinaifanya mkoa huo kuwa na
fursa nyingi za kiuchumi.
Aidha amesema upatikanaji wa huduma muhimu kama umeme,
maji na miundombinu ya barabara umeendelea kuboresha maisha ya wananchi na
kuvutia wawekezaji katika sekta mbalimbali.
Katika hotuba yake, Mkuu huyo wa Mkoa amempongeza Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea
kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo imechangia
kuboresha huduma kwa wananchi.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa MISA Tanzania, Edwin
Soko, amesema kongamano hilo linalenga kuimarisha ushirikiano kati ya vyombo
vya habari na wadau wa maendeleo pamoja na kuendeleza uandishi wa habari
unaolenga kutoa suluhisho kwa changamoto za jamii.
Soko amesema MISA Tanzania itaendelea kulinda uhuru wa
vyombo vya habari, uhuru wa kujieleza na haki ya kupata taarifa, huku
akiwahimiza waandishi wa habari kuendelea kuandika wenye suluhisho kwa
kuzingatia weledi wao.
Aidha ameeleza kuwa taasisi hiyo ina mpango wa
kuanzisha kituo cha ugawaji wa taarifa za maendeleo kwa jamii, ambacho kitatoa
elimu na taarifa muhimu kwa wananchi, na kuiomba serikali ya mkoa kutoa eneo la
ardhi kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa amekubali ombi hilo na kusema
serikali ya mkoa iko tayari kushirikiana na MISA Tanzania kwa kutoa eneo la
kujenga kituo hicho cha taarifa.
Katika hatua nyingine, Meneja wa NSSF Mkoa wa Iringa,
Benedict Wela, amesema taasisi hiyo inaendelea kuwahamasisha Watanzania
kujiunga na mfumo wa hifadhi ya jamii ili kuwasaidia kujikinga na umaskini na
kuwa na usalama wa kipato baada ya kustaafu.
Kongamano hilo limewakutanisha waandishi wa habari,
wahariri, viongozi wa serikali pamoja na wadau mbalimbali kwa lengo la kujadili
mchango wa sekta ya habari katika maendeleo ya Mkoa wa Iringa na taifa kwa
ujumla.
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254





















































































































Post a Comment