Na Edington Mukiza Ezron, Misalaba Media
Baadhi ya vijana katika Manispaa ya Shinyanga
wameiomba serikali kuwawezesha kwa kuwapatia fursa mbalimbali za kiuchumi,
ikiwemo mikopo yenye masharti nafuu, zabuni, pamoja na kushirikishwa katika
miradi ya maendeleo ili waweze kujipatia kipato na kujikwamua kimaisha.
Wakizungumza na Misalaba Media leo Machi 27, 2026
katika nyakati tofauti, vijana hao wameeleza kuwa changamoto ya ukosefu wa
ajira bado ni kubwa, na kwamba hali hiyo inahitaji juhudi za pamoja kati ya
serikali na jamii kwa ujumla ili kuipunguza na hatimaye kuimarisha maisha ya
vijana.
Mmoja wa vijana hao, Zephania Tulinge Lucas, mkazi wa
Kata ya Ngokolo, amesema ukosefu wa ajira umesababisha baadhi ya vijana
kujiingiza katika vitendo visivyofaa ikiwemo wizi, matumizi ya dawa za kulevya
pamoja na kukata tamaa ya kuendelea na masomo kutokana na kutokuona manufaa ya
elimu.
Kwa upande wake, Joseph Steven amesema serikali haina
budi kuongeza uwekezaji utakaosaidia kutoa ajira kwa vijana, pamoja na kuweka
mikopo yenye riba nafuu ili kuwawezesha kuanzisha na kuendesha biashara zao.
Aidha, amewashauri vijana kujishughulisha na shughuli
mbalimbali za kujipatia kipato badala ya kusubiri ajira rasmi, ili waweze
kuendesha maisha yao.
Naye Magreth Charles Marwa amesema vijana wanapaswa
kuwa wabunifu na kutojikita tu kwenye elimu waliyonayo, bali kutafuta fursa
mbalimbali zitakazowawezesha kujikwamua kiuchumi na kuepuka kujiingiza katika
vitendo vya uhalifu.
Ameongeza kuwa ni muhimu kwa serikali kuweka mazingira
rafiki kwa vijana kwa kutoa ajira ndogo ndogo, mikopo ya biashara pamoja na
elimu ya ujasiriamali.
Hata hivyo, amewataka vijana wasio na ajira kuwa
wavumilivu huku wakijishughulisha na shughuli mbalimbali wanazosubiri fursa za
ajira serikalini, ili waweze kutimiza ndoto zao.
Aidha, vijana hao wameeleza kuwa licha ya kuwepo kwa
mikopo na fursa mbalimbali zinazotolewa na serikali, bado elimu kuhusu
upatikanaji na taratibu zake haijawafikia moja kwa moja, hali inayowafanya
wengi kushindwa kunufaika na fursa hizo kutokana na ukosefu wa taarifa sahihi.
SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment