" WATU 18 WAFARIKI, 5 WAJERUHIWA KATIKA MAAFA MAKUBWA MBEYA

WATU 18 WAFARIKI, 5 WAJERUHIWA KATIKA MAAFA MAKUBWA MBEYA


TAARIFA KWA UMMA

 

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linaendelea kuimarisha ulinzi na usalama wa raia na mali zao kwa kufanya misako na doria katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Mbeya hali inayopelekea Amani na Utulivu.

 

Tarehe 25.03.2026 kati ya saa 6 hadi saa 9:30 usiku katika Kata ya Nkunga, Lupepo, Kawetele na Ikuti Wilayani Rungwe, Mkoa wa Mbeya, mvua kubwa iliyoambatana na upepo ilinyesha na kusababisha vifo vya watu 18 kati yao watu wazima ni 04 [wanawake 3 na mwanaume 1] na watoto waliofariki dunia ni 14 [wa kike 8 na wa kiume 6].

 

Mvua hiyo iliyoambatana na upepo mkali ilisababisha nyumba zaidi ya 9 zilizojengwa kwa tofali mbichi na kuezekwa bati kusombwa na maporomoko ya udongo mzito na kusababisha vifo hivyo. Walifariki katika maafa hayo ni Chapakazi Mwasota [60], Rhoida Mwangwina [55], Gladness Chapakazi [18], Neema Mwasyema [31], Aneth Morohan [35], Obeid Shibuka [20] na Itika Manyanya [26].

 

Watoto waliofariki katika Maafa hayo ni Vivian Ahonga, mwaka 1, Briana Mwachiombo [3], Dailan Kasambala [6] aliyekuwa Mwanafunzi wa Chekechea katika Shule ya Msingi Lupepo, Innoent Kasambala [4], Vivian Andrea [13] aliyekuwa Mwanafunzi Darasa la Saba katika Shule ya Msingi Lupepo, Princess Ibrahim [5] aliyekuwa Mwanafunzi wa Chekechea katika Shule ya Msingi Lupepo, Nathanael Christopher [2], Jonathan Hamis, miezi kumi, Irine Anangisye [16] aliyekuwa Mwanafunzi wa Kidato cha Tatu katika Shule ya Sekondari Lupepo, Wema Hamis [5] aliyekuwa Mwanafunzi wa Chekechea katika Shule ya Msingi Kikuyu na Kenedy Mahenge [14], aliyekuwa Mwanafunzi wa Kidato cha Pili Sekondari ya Ikuti.

 

Aidha, katika Maafa hayo watu 5 walijeruhiwa kati yao watoto 3 wa kike na watu wazima 2, mwanaume 1 na mwanamke 1. Majeruhi wanaendelea kupatiwa matibabu katika Hospitali ya Wilaya Makandana – Tukuyu na Zahanati ya Chuo cha Magereza Kiwira.

 

 

 

 

 

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya kwa kushirikiana na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji linaendelea na kazi ya Uokoaji katika maeneo hayo.  Aidha, timu za Madaktari zipo maeneo hayo kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa kitabibu wa miili ya marehemu na kutoa huduma za awali kwa wahanga. Kamati ya Maafa ya Wilaya pia inaendelea na tathimini ya matukio hayo na kutoa misaada kwa wahanga wengine wakazi wa maeneo hayo.

 

Wakati huo huo, Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linamshikilia Gilbert Edwin Mwabulesi [26] mkazi wa Ibililo Wilayani Rungwe Mkoa wa Mbeya kwa tuhuma za mauaji ya baba yake mzazi aitwaye Edwin Mwabulesi [65] aliyekuwa mkazi wa Kijiji cha Ibililo kwa kumpiga sehemu mbalimbali za mwili.

 

Tukio hilo lilitokea Machi 21, 2026 saa 9:20 usiku katika Kitongoji cha Nsanga, Kijiji cha Ibililo, Kata ya Nkunga, Tarafa ya Ukukwe, Wilaya ya Rungwe, Mkoa wa Mbeya baada ya mtuhumiwa Gilbert Mwabulesi kumshambulia kwa kumpiga ngumi na mateke sehemu mbalimbali za mwili baba yake mzazi aitwaye Edwin Mwabulesi na kusababisha kifo chake.

 

Uchunguzi wa awali umebaini kuwa chanzo cha tukio ni mzozo wa kifamilia uliotokea baina yao ambapo mtuhumiwa anaishi na wazazi wake, hivyo baada ya kurudi kutoka matembezini alianza kugonga mlango kwa fujo akipiga kelele na kutokana na vitendo hivyo baba yake mzazi aliamka na kumfuata kwa lengo la kumuonya ndipo alianza kumshambulia kwa kumpiga hadi kufariki dunia.

 

Taratibu za kisheria zinakamilishwa ili mtuhumiwa afikishwe mahakamani kwa hatua zaidi za kisheria.

 

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linatoa wito kwa wananchi kuchukua tahadhari kipindi hiki cha mvua za masika zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Mbeya ili kuepuka madhara. Aidha, Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linatoa wito kwa baadhi ya vijana kuacha matumizi ya dawa za kulevya na kupelekea kufanya uhalifu.

 

imetolewa na:

Kamanda wa Polisi,

Mkoa wa Mbeya.


Post a Comment

Previous Post Next Post