" SIAGI: AMANI ILIYOPO NCHINI NI TUNU MUHIMU KWA KILA MTANZANIA

SIAGI: AMANI ILIYOPO NCHINI NI TUNU MUHIMU KWA KILA MTANZANIA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi CCM Mkoa wa Shinyanga, Bwana John Siagi, amewakumbusha viongozi wa Seneti Mkoa wa Shinyanga kuendelea kuwa mabalozi wazuri wa kusimamia amani na utulivu katika maeneo yao.

Siagi ametoa wito huo wakati wa kikao cha pamoja, ambapo ameeleza kwa ufupi historia ya Tanzania tangu ilipopata uhuru na namna ilivyoendelea kuwa nchi ya amani, akibainisha kuwa hali hiyo imejengwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

Amesema kuwa amani iliyopo nchini ni tunu muhimu inayopaswa kulindwa na kila Mtanzania, huku akisisitiza kuwa viongozi wa serikali wameendelea kuisimamia kwa ufanisi na kuhakikisha inaendelea kudumu.

Aidha, amesema Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Shinyanga itaendelea kushirikiana na viongozi mbalimbali katika kutekeleza majukumu yao, ikiwa ni pamoja na kuendeleza amani kwa mujibu wa ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Seneti Mkoa wa Shinyanga, Bwana Jackson Aloyce Mwizarubi, amesema yeye pamoja na viongozi wengine wa Seneti wataendelea kusimamia sheria na taratibu za nchi ili kuhakikisha amani inalindwa wakati wote.

Ameongeza kuwa endapo kutajitokeza viashiria vyovyote vya uvunjifu wa amani, watatoa taarifa kwa mamlaka husika ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa mapema.

Mwizarubi pia amebainisha kuwa kuanzia Aprili 17, 2026, viongozi wa Seneti Mkoa wa Shinyanga wameanza ziara ya kutembelea vyuo mbalimbali mkoani humo, kwa lengo la kuwasaidia vijana kutambua fursa zilizopo, kusikiliza changamoto zao na kuimarisha uongozi katika ngazi za matawi.

Kwa pamoja, viongozi hao wamehimiza vijana na wananchi kwa ujumla kuendelea kulinda amani, kuheshimu sheria na kushiriki katika shughuli za maendeleo ili kudumisha ustawi wa jamii na taifa kwa ujumla.


 

Post a Comment

Previous Post Next Post