" VIONGOZI WA JMAT SHINYANGA WAKEMEA HUJUMA, WASISITIZA AMANI NA ULINZI WA MIUNDOMBINU

VIONGOZI WA JMAT SHINYANGA WAKEMEA HUJUMA, WASISITIZA AMANI NA ULINZI WA MIUNDOMBINU

 

Na Mapuli Kitina Misalaba

Viongozi wa Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT) Mkoa wa Shinyanga wameonya vikali vitendo vya hujuma dhidi ya miundombinu ya ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Shinyanga, wakisisitiza kuwa kulinda miradi ya maendeleo ni sehemu ya kudumisha amani na ustawi wa jamii.

Onyo hilo limetolewa kufuatia ziara ya viongozi hao katika mradi huo ambapo walijionea hatua ya utekelezaji wake, huku ujenzi ukiwa umefikia asilimia 97.3 ya ukamilishaji.

Akizungumza mara baada ya ziara hiyo, Mwenyekiti wa JMAT Mkoa wa Shinyanga, Sheikh Balilusa Khamisi, amesema kuwa wataendelea kutumia majukwaa ya kidini kuhubiri amani, uzalendo na kuwahimiza wananchi kulinda mali za umma ili kukomesha vitendo vya wizi na uharibifu wa miundombinu.

Amesema vitendo vya hujuma vinahatarisha juhudi za serikali katika kuwaletea wananchi maendeleo, akibainisha kuwa serikali imewekeza fedha nyingi katika miradi hiyo kwa manufaa ya wote. Ameongeza kuwa kukamilika kwa uwanja huo kutafungua fursa nyingi za kiuchumi na kibiashara kwa wakazi wa mkoa wa Shinyanga.

Viongozi hao wa JMAT wamesema utekelezaji wa mradi huo unaonyesha dhamira ya dhati ya serikali katika kupanga, kuwekeza na kusimamia miradi ya maendeleo kwa ufanisi, hivyo ni wajibu wa wananchi kushirikiana kuulinda.

Kwa upande wake, msimamizi wa uwanja huo, Lugano Mwinuka, akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Abdul Athuman Mombokaleo, amesema mradi huo unatarajiwa kukamilika hivi karibuni na utaimarisha huduma za usafiri wa anga ndani na nje ya mkoa huo.

Amesema kukamilika kwa uwanja huo kutaongeza fursa za biashara, kuchochea shughuli za kiuchumi na kuongeza mapato ya serikali kupitia kodi na tozo mbalimbali.

Hata hivyo, Mwinuka amebainisha kuwepo kwa changamoto ya wizi wa miundombinu, akieleza kuwa Januari mosi mwaka huu watu wasiojulikana waliiba baadhi ya vyuma vya uzio wa uwanja huo, hali inayohitaji ushirikiano wa wananchi na vyombo vya ulinzi na usalama kukomesha vitendo hivyo.

Naye Mhandisi Chiyando Matoke, akizungumza kwa niaba ya Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), amesema mradi huo unatekelezwa kwa gharama ya shilingi bilioni 44.8, ambapo hadi sasa serikali imelipa shilingi bilioni 38.6 kwa mkandarasi.

Ametumia nafasi hiyo kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuwekeza katika miradi ya miundombinu inayochochea ukuaji wa uchumi na kuboresha huduma za kijamii nchini, ikiwemo mkoa wa Shinyanga.

Aidha, ameeleza kuwa serikali tayari imelipa fidia kwa wananchi wote waliopisha utekelezaji wa mradi huo.

Mradi wa ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Shinyanga unafadhiliwa na Serikali ya Tanzania na unatekelezwa na mkandarasi wa China, Hennan International Corporation Group Co. Ltd (CHICO), huku ukitarajiwa kuwa chachu ya maendeleo na ustawi wa kiuchumi katika mkoa huo.

 


 SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA

 
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment

Previous Post Next Post