" WIZI, DAWA ZA KULEVYA NA FEDHA BANDIA: WATUHUMIWA 63 WAKAMATWA SHINYANGA

WIZI, DAWA ZA KULEVYA NA FEDHA BANDIA: WATUHUMIWA 63 WAKAMATWA SHINYANGA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Jumla ya watuhumiwa 63 wamekamatwa kwa makosa mbalimbali mkoani Shinyanga kufuatia operesheni zilizofanywa na Jeshi la Polisi katika kipindi cha mwezi Aprili 2026.

Kwa mujibu wa Kamanda wa jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga kamishna msaidizi mwandamizi wa Polisi Janeth Magomi, operesheni hizo zililenga kukabiliana na uhalifu na kudhibiti vitendo vinavyokiuka sheria ambapo zimefanikisha kukamatwa kwa watuhumiwa hao pamoja na kukamatwa kwa vielelezo mbalimbali.

Vielelezo vilivyokamatwa ni pamoja na mafuta ya dizeli lita 295, bangi gramu 1,100, mirungi kilogramu 103, noti bandia zenye thamani ya shilingi 81,000, simu 98, betri za simu 86, pomba na moshi lita 55, pikipiki 14, vipande vya chuma 21, redio 8, viti vya plastiki 6, mifuko 13 ya mawe yanayodhaniwa kuwa madini, spika 5, mashine ya kukatia mikate 1 na mbuzi 7 waliokamatwa katika wilaya za Kahama na Ushetu.

Aidha, polisi wamesema kesi saba zimefikishwa mahakamani ambapo watuhumiwa saba wamehukumiwa kifungo cha miezi sita hadi miaka minne jela katika kesi za wizi. Kesi nyingine zinahusisha kutishia kwa maneno, kushambulia na kudhuru mwili, pamoja na kuharibu mali, ambapo wahusika wamehukumiwa vifungo mbalimbali jela.

Katika hatua nyingine, Kikosi cha Usalama Barabarani kimeendelea na operesheni dhidi ya madereva wanaokiuka sheria za usalama barabarani, ambapo jumla ya makosa 4,260 yalibainika. Miongoni mwa makosa hayo ni ya magari 3,030 pamoja na makosa ya bajaji na pikipiki 1,230, huku wahusika wakitozwa faini katika maeneo husika.

Polisi pia wamemfungia leseni dereva mmoja kwa muda wa miezi mitatu baada ya kukutwa akiendesha gari kwa mwendokasi wa zaidi ya kilomita 80 kwa saa.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga limewataka wananchi kuendelea kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kwa kutoa taarifa zitakazosaidia kukomesha uhalifu na kuimarisha amani katika jamii.

SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254


Post a Comment

Previous Post Next Post