Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mboni Mhita, akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kuanza kwa kampeni ya Samia Legal Aid itakayotoa msaada wa kisheria bure kuanzia Mei 6 hadi Mei 20, 2026 mkoani humo.Na Mapuli Kitina Misalaba
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mboni Mhita, ametangaza
kuanza kwa utekelezaji wa kampeni ya kitaifa ya Samia Legal Aid mkoani humo,
itakayotoa huduma za msaada wa kisheria bure kwa wananchi kwa kipindi cha wiki
mbili kuanzia Mei 6 hadi Mei 20, 2026.
Akizungumza na vyombo vya habari Mei 5, 2026, Mhita
amesema kampeni hiyo inalenga kuwafikia wananchi wengi zaidi kwa kuwapeleka
wataalamu wa sheria katika kata zote 130 za mkoa huo, ili kusaidia utatuzi wa
migogoro na changamoto mbalimbali za kisheria zinazowakabili.
Ameeleza kuwa huu ni mwendelezo wa jitihada za
Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha haki
inapatikana kwa urahisi, huku wananchi wakiepuka gharama za kufuata huduma za
kisheria mbali na maeneo yao.
Ameongeza kuwa kampeni hiyo ni awamu ya pili kufanyika
mkoani Shinyanga, ambapo katika awamu ya kwanza iliyotekelezwa mwaka 2023,
jumla ya migogoro 578 ilishughulikiwa na kati yake 378 ilifanikiwa kutatuliwa,
huku zaidi ya wananchi 22,000 wakinufaika na huduma hiyo.
Kwa mujibu wa Mhita, huduma zitakazotolewa katika
kampeni hiyo ni pamoja na ushauri wa kisheria, utoaji wa elimu kwa umma kuhusu
masuala ya sheria, uandaaji wa nyaraka mbalimbali za kisheria na uwakilishi
katika vyombo vya utoaji haki.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi wa Huduma za
Uzingatiwaji wa Msaada wa Kisheria, Osborn Paissi, amesema kampeni hiyo
inalenga pia kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu haki zao na namna bora ya
kuzilinda kupitia mifumo rasmi ya kisheria.
Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Kisheria Mkoa wa
Shinyanga, John Shija, amesema wanatarajia mafanikio makubwa katika awamu hii
ya pili, akibainisha kuwa huduma hizo zitawafikia wananchi wa makundi yote na
kuchangia kupunguza migogoro katika jamii.
Ametoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi
kushiriki kampeni hiyo ili kunufaika na huduma hizo muhimu, ambazo zitaleta
suluhisho la kudumu kwa changamoto za kisheria zinazowakabili.
SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254
Post a Comment