Na Mapuli Kitina Misalaba
Mwandishi wa habari kutoka Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Shinyanga (Shinyanga Press Club)SPC, Stella Ibengwe, amesema maadhimisho ya World Press Freedom Day ni fursa muhimu kwa wanahabari kujikumbusha wajibu wao wa kutekeleza majukumu kwa weledi na kuzingatia maadili ya taaluma.
Ibengwe amesema siku hiyo ina umuhimu mkubwa kwa
waandishi wa habari kwani inawakumbusha wajibu wao wa kuhakikisha wanaripoti
habari sahihi, zenye uwiano na zinazozingatia maadili ya uandishi wa habari.
Ameeleza kuwa kuongezeka kwa matumizi ya mitandao ya
kijamii kumechangia kusambaa kwa taarifa zisizo sahihi, akibainisha kuwa baadhi
ya watu wamekuwa wakijichukulia jukumu la kuripoti matukio bila kufuata misingi
ya taaluma hiyo.
“Kuna tofauti kati ya mwandishi wa habari
mtaalamu na mtu wa kawaida anayerekodi tukio na kusambaza bila kuthibitisha
taarifa. Hali hii imekuwa ikisababisha kusambaa kwa habari zisizo sahihi na
wakati mwingine kuleta taharuki katika jamii,”
amesema Ibengwe.
Ameongeza kuwa mwandishi wa habari mtaalamu hawezi
kuripoti habari zinazoweza kusababisha taharuki kwa jamii, badala yake
huzingatia ukweli, usahihi na maadili ya kazi yake.
Aidha, ameiomba serikali kuendelea kuchukua hatua kali
dhidi ya watu wanaosambaza taarifa za uongo kwenye mitandao ya kijamii, akisema
vitendo hivyo vinaweza kuleta athari kubwa kwa jamii na taifa kwa ujumla.
“Serikali iendelee kuchukua hatua kwa wale
wanaosambaza habari za uongo zinazoweza kusababisha mtafaruku na kuvuruga
utulivu wa jamii,” amesisitiza.
Pia amewataka wadau mbalimbali kuendelea kushirikiana
na vyombo vya habari ili kuhakikisha taarifa sahihi zinawafikia wananchi kwa
wakati na kwa usahihi, akieleza kuwa ushirikiano huo ni muhimu katika kuleta
maendeleo ya taifa.
“Ni muhimu kwa wadau kuendelea kutoa
ushirikiano kwa waandishi wa habari ili tuweze kutimiza jukumu letu la
kuhabarisha jamii kwa kina na kwa usahihi,” amesema.
Ibengwe amesisitiza kuwa lengo la waandishi wa habari
ni moja, ambalo ni kuchangia maendeleo ya nchi kupitia utoaji wa taarifa sahihi
na zenye manufaa kwa jamii.
SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment