
Na Happy Lazaro, Arusha
Katika jitihada za kuendelea kuboresha huduma zinazotolewa kwa watalii wanaotembelea Tanzania, Zara Tanzania Adventures imeendesha mafunzo maalumu ya kuwajengea uwezo Maafisa wa Polisi wa Utalii kutoka maeneo mbalimbali nchini.
Mafunzo hayo yamejikita katika kuongeza uelewa kuhusu huduma kwa wateja, nafasi ya utalii katika kukuza uchumi wa taifa, mawasiliano yenye tija, pamoja na mbinu bora za kuhudumia wageni wa ndani na wa kimataifa.
Kupitia mafunzo hayo, maafisa wamekumbushwa kuwa jukumu lao linaenda mbali zaidi ya kulinda usalama.
” Kwa mwenendo wao, maadili yao na namna wanavyowapokea na kuwahudumia wageni, wanakuwa sura ya kwanza ya Tanzania na huchangia kwa kiasi kikubwa taswira ya nchi kama kivutio salama na chenye ukarimu.”
Kama sehemu ya programu hiyo, maafisa hao wanatarajiwa kutembelea Hoteli ya Springlands ili kujifunza kwa karibu historia na mafanikio ya Zara Tanzania Adventures katika kipindi cha miaka 40 ya utoaji wa huduma za utalii.
Ziara hiyo pia itatoa nafasi ya kufahamu mchango wa kampuni katika utalii endelevu, uhifadhi wa mazingira na wanyamapori, pamoja na miradi ya kuwawezesha wananchi kiuchumi.
Ushirikiano kati ya sekta binafsi na vyombo vya usalama unaendelea kuwa nguzo muhimu katika kuimarisha tasnia ya utalii nchini.
Kupitia ushirikiano huo, Tanzania inaendelea kujenga mazingira salama, yenye huduma bora na yanayovutia watalii kutoka sehemu mbalimbali duniani

Post a Comment