" MWENGE WA UHURU WAFURAHISHWA NA MIRADI 7 YA MAENDELEO KATIKA MANISPAA YA SHINYANGA

MWENGE WA UHURU WAFURAHISHWA NA MIRADI 7 YA MAENDELEO KATIKA MANISPAA YA SHINYANGA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Mwenge wa Uhuru ukiongozwa na Mkimbiza Mwenge Kitaifa, Wazo Marco Mwang’onda, umeendelea na shughuli zake katika Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga kwa kuzindua, kuweka mawe ya msingi na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 5.2.

Katika ziara hiyo, Mwenge wa Uhuru umefikia miradi mbalimbali katika sekta za afya, maji, elimu, nishati, uwezeshaji wananchi kiuchumi na miundombinu, ambapo mwenge wa uhuru umetamka  kuwa miradi hiyo imekidhi viwango na imepitishwa kwa ajili ya matumizi ya wananchi.

Akizungumza wakati wa hafla hizo, Mkimbiza Mwenge Kitaifa, Wazo Marco Mwang’onda, amesema Mwenge wa Uhuru unaendelea kuwa chombo muhimu katika kuhamasisha wananchi kushiriki katika shughuli za maendeleo, kusimamia matumizi sahihi ya fedha za umma na kuhakikisha miradi inayotekelezwa inawanufaisha wananchi.

Amesema ziara hiyo inalenga pia kuwakumbusha wananchi umuhimu wa kutunza na kutumia vizuri miradi inayotekelezwa kwa fedha za Serikali pamoja na kuendelea kushirikiana na viongozi katika kusukuma mbele maendeleo ya maeneo yao.

Katika ziara hiyo, Mwenge wa Uhuru umezindua mradi wa maji safi katika Kitongoji cha Mwamala, ukiwa ni miongoni mwa miradi inayolenga kuboresha upatikanaji wa huduma ya maji kwa wananchi wa eneo la kata ya Kolandoto.

Mwenge pia umefungua mradi wa Zahanati ya Mwagala, iliyopo Kata ya Ibadakuli, wenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 100.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa zahanati hiyo, Mwang’onda ameeleza umuhimu wa uwepo wa huduma za afya karibu na wananchi, huku akimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuimarisha miundombinu ya afya nchini.

Baadhi ya wananchi wa Mwagala wameishukuru Serikali kwa kuhakikisha mradi huo unakamilika na kuanza kutoa huduma kwa jamii.

Katika hatua nyingine, Mwenge wa Uhuru umeweka jiwe la msingi katika Makindo Hotel, mradi ambao ni miongoni mwa uwekezaji unaolenga kuchochea shughuli za kiuchumi na kuongeza fursa za ajira na biashara katika Manispaa ya Shinyanga.

Mwenge pia umefikia Kikundi cha Mkasa Fashion, kinachoundwa na vijana ambao ni wanufaika wa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa kupitia mapato ya ndani ya Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga.

Aidha, Mwenge wa Uhuru umezindua mradi wa nishati safi ya kupikia, unaosimamiwa na Taasisi ya Wanawake na Samia Mkoa wa Shinyanga, ukiwa na lengo la kuhamasisha matumizi ya nishati safi na salama ya kupikia.

Katika sekta ya miundombinu Mwenge wa uhuru umeweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa Daraja la Dodoma, lililopo Kata ya Ndembezi na kwamba mradi huo una thamani ya zaidi ya shilingi milioni 100.

Mwenge pia umetembelea na kukagua ukarabati wa vyumba vinne vya madarasa katika Shule ya Sekondari Old Shinyanga, hatua inayolenga kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia kwa wanafunzi.

Katika shughuli hizo, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini, Paschal Patrobas Katambi, ameshiriki katika shughuli za mapokezi na ufuatiliaji wa ziara ya Mwenge wa Uhuru, akisisitiza umuhimu wa Serikali na wananchi kuendelea kushirikiana katika kuleta maendeleo.

Mwenge wa Uhuru unaendelea na shughuli zake mkoani Shinyanga, ambapo unatarajiwa kuendelea na ziara katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, huku ukibeba kauli mbiu inayosema:

“TANZANIA NI YETU SOTE, TUSHIKAMANE KWA PAMOJA KULETA MAENDELEO.”











 

Post a Comment

Previous Post Next Post