" CHIFU ANTONIA SANGALALI AWATAKA WANANCHI KUTUNZA NOTI, ASISITIZA UJUMBE WA BENKI KUU YA TANZANIA

CHIFU ANTONIA SANGALALI AWATAKA WANANCHI KUTUNZA NOTI, ASISITIZA UJUMBE WA BENKI KUU YA TANZANIA

Mwenyekiti wa Machifu Tanzania na Mtemi wa Himaya ya Jigoku, Chifu Antonia Sangalali, amewataka wananchi kuhakikisha wanatunza fedha za Tanzania kwa kuepuka kuzichana, kuzitoboa au kuziandikia, akisisitiza kuwa noti hizo hutumika na watu mbalimbali katika mzunguko wa fedha.

Chifu Sangalali ametoa ujumbe huo wakati wa Tamasha la 19 la Himaya ya Jigoku, Masela, Wilaya ya Maswa mkoani Simiyu, akisema amepokea ujumbe kutoka Benki Kuu ya Tanzania na kuamua kuufikisha kwa wananchi kupitia nafasi yake kama Mwenyekiti wa Machifu Tanzania.

Amesema wananchi wanapaswa kutambua kuwa noti wanazoshika leo zinaweza kutumika na mtu mwingine kesho, hivyo ni muhimu kuzitunza ili ziendelee kuwa katika hali nzuri na kutumika katika shughuli mbalimbali za kiuchumi.

“Benki Kuu ya Tanzania ina ujumbe kwa Watanzania wote kupitia kwangu mimi nikiwa kama Mwenyekiti wa Machifu Tanzania. Mzitunze pesa za Tanzania, msizichane, msizitoboe, msiziandike,” amesema Chifu Sangalali.

Ameongeza kuwa fedha ni mali inayozunguka katika jamii, hivyo kila mwananchi ana wajibu wa kuhakikisha anaitunza kwa usalama na heshima.

Ujumbe huo umetolewa sambamba na wito wa Chifu Sangalali kwa wananchi kuendelea kudumisha amani, mshikamano na maadili, akisisitiza umuhimu wa kila mmoja kuwa na wajibu wa kulinda ustawi wa jamii na taifa kwa ujumla.

Tamasha hilo la 19 la Himaya ya Jigoku limewakutanisha ndugu wa utemi kutoka maeneo mbalimbali nchini Tanzania pamoja na wageni kutoka Uganda, huku likinogeshwa na burudani za ngoma za asili.

Mwenyekiti wa machifu Tanzania Mtemi Antonia Sangalali akishiriki kwenye kikao cha pamoja na viongozi wa benki kuu ya Tanzania.



 

Post a Comment

Previous Post Next Post