" MWANA FA AZINDUA MASHINDANO YA AWESO CUP 2026

MWANA FA AZINDUA MASHINDANO YA AWESO CUP 2026



NA: MWANDISHI WETU, PANGANI

Mashindano ya mpira wa miguu ya Aweso Cup 2026 - Wekeza Pangani, yanayodhaminiwa na Mbunge wa Jimbo la Pangani na Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, yamezinduliwa rasmi na Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamisi Mwinjuma (Mwana FA).

Uzinduzi huo umefanyika Septemba 12, 2026, katika uwanja wa Casablanca, Sakura wilayani humo, ambapo wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya wilayani humo walijitokeza kushuhudia uzinduzi huo wa aina yake.

Katika tukio hilo, Naibu Waziri Mwinjuma, alimpongeza Aweso kwa kuwa mdau wa michezo kwani udhamini huo ni ishara tosha kuwa anathamini vipaji vya michezo.

"Nampongeza Mbunge wenu Aweso kwa uwekezaji huu alioufanya, siku hizi michezo ni fursa ya kujipatia kipato, hivyo niwahimize wachezaji kujituma na kuonyesha vipaji vyenu kwani itakuwa njia ya  kujipatia kipato," amesema Mwinjuma.

Naye, Msemaji wa Timu za Taifa za Tanzania, Haji Manara, amesema serikali inawekeza katika michezo kwani michezo ni fursa ya kukuza vipaji, kujenga afya na kupata kipato na hivyo kuchangia ujenzi wa taifa.

Katika hatua nyingine, Aweso ambaye ndiye mdhamini wa mashindano hayo, amesema dhamira yake ya kuinua michezo wilayani humo ipo pale pale, hivyo vijana wajipange kutumia michezo kubadili maisha yao.


"Nitaendelea kuweka nguvu kubwa kuinua michezo Pangani kwani Ina mchango mkubwa katika maendeleo ya mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla. Udhamini huu utaendelea ili Pangani iwe kinara wa michezo hapa nchini".

Ikumbukwe kuwa, mashindano hayo yanajumuisha timu 80 za wilayani humo, huku zawadi nono zikitarajiwa kutolewa kwa washindi.  

Ni kwamba, mshindi wa kwanza wa mashindano hayo atajinyakulia kitita cha shilingi milioni kumi, wapili milioni tano na watatu milioni tatu, huku shabiki bora akijinyakulia pikipiki mpya. 

Pamoja na michezo hiyo, hamasa inatolewa juu ya umuhimu wa kuwekeza katika sekta mbalimbali ili kuchochea maendeleo.

 PROFESSOR MGOKO SERIES (EP 1)

Post a Comment

Previous Post Next Post