Serikali imeutaka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kujipanga kikamilifu katika maandalizi ya mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027, hususan katika kuhakikisha wageni watakaofika nchini wanapata huduma bora za matibabu bila vikwazo.
Agizo hilo limetolewa l na Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Florence Samizi (Mb.) ambaye amesema NHIF ina jukumu muhimu la kuratibu suala la bima ya afya wakati wa mashindano hayo ili kuhakikisha wageni wanapata huduma za matibabu kwa urahisi pindi wanapohitaji huduma hizo.
“Tuwape uhakika wa huduma bora ili waone fahari kuwapo hapa nchini katika kipindi chote cha mashindano hayo,” amesema Dkt. Samizi.
Amesema maandalizi ya huduma za matibabu yanapaswa kuzingatia pia huduma za dharura pamoja na huduma maalum, ikiwemo za moyo na mifupa, ili kukidhi mahitaji mbalimbali ya afya yatakayoweza kujitokeza wakati wa mashindano.
Aidha alidokeza kuwa tayari Wataalamu kutoka Shirikisho la Soka Afrika (CAF) wamekagua Vituo vya kutolea huduma kwa alengo la kujiridhisha na wamefurahishwa na utayari unaoonyeshwa katika maandalizi ya huduma za matibabu jambo linaloonesha kuwa Tanzania inajiandaa kuhakikisha AFCON 2027 inafanyika katika mazingira salama na yenye huduma bora.
Ameitaka NHIF kushirikiana kwa karibu na Wizara ya Afya, vituo vya kutolea huduma na wadau wengine kuhakikisha mfumo wa huduma za matibabu wakati wa mashindano hayo unakuwa imara, unaopatikana kwa wakati na unaokidhi viwango vinavyohitajika.
Akizungumzia hilo Mkurugenzi Mkuu waa NHIF, Dkt. Irene Isaka alisema kuwa tayari Mfuko umeshajipanga na umeandaa kifurushi maalumu kwa ajili ya wageni wote watakaokuja nchini kwa ajili ya mashindano hayo.
“Tayari tumejipanga na tuna kifurushi ambacho tutakileta Wizarani ili tupate baraka ya Wizara hivyo tunashukuru sana kwa maelekezo haya ambayo yanaboresha na kuhakikisha tunajipanga vyema,” alisema Dkt. Isaka.
Post a Comment