" ASKOFU WA JIMBO LA SHINYANGA LIBERATUS SANGU, KESHO ATAWEKA WAKFU MAFUTA YA KRISMA TAKATIFU NA KUBARIKI MAFUTA YA WAGONJWA NA WAKATEKUMENI.

ASKOFU WA JIMBO LA SHINYANGA LIBERATUS SANGU, KESHO ATAWEKA WAKFU MAFUTA YA KRISMA TAKATIFU NA KUBARIKI MAFUTA YA WAGONJWA NA WAKATEKUMENI.

 Askofu wa Kanisa Katoliki Jimbo la Shinyanga Mhashamu Liberatus Sangu, kesho Jumanne tarehe 28.03.2023, ataweka wakfu Mafuta ya Krisma takatifu, pamoja na kubariki mafuta ya wagonjwa na Wakatekumeni.

Misa ya Krisma ambayo itaanza saa 4:00 asubuhi, itafanyika katika Kanisa kuu la Mama mwenye Huruma Ngokolo mjini Shimyanga, na itahudhuriwa na Mapadre kutoka katika Parokia zote za Jimbo, pamoja na waamini.

 Kupitia Misa hiyo, Mapadre wote watarudia viapo vyao vya kipadre mbele ya Askofu wa Jimbo, na baadaye waamini watapata nafasi ya kuwapongeza kwa majitoleo waliyoyafanya kupitia huduma za kiroho walizowapatia, katika kipindi cha mwaka mzima.

 Mafuta ya Krisma ambayo huwekwa Wakfu na Askofu wa Jimbo mbele ya Mapadre na waamini siku chache kabla ya adhimisho la Pasaka, hutumiwa na Kanisa kwa ajili ya kutakatifuza wakati wa utoaji wa Sakramenti mbalimbali za Kanisa, ambazo ni pamoja na Ubatizo, Kipaimara na Sakramenti ya Daraja (Ushemasi, Upadre na Uaskofu)

Mafuta hayo pia hutumika kutakatifuza vifaa mbalimbali vinavyotumika kwa kazi za ibada na Misa takatifu, ikiwemo Kanisa, Altare na Kalisi.

 Kwa upande wa mafuta ya wagonjwa, wanapakwa ili kuwatia neema maalum, kuwapa nguvu na kuwafariji katika ugonjwa wao, pamoja na kuwaandaa kwa ajili ya kukutana na Mwenyezi Mungu.

 Aidha, mafuta ya Wakatekumeni hupakwa wanafunzi wa dini kabla ya kupewa Sakramenti ya ubatizo, ili kuwaimarisha katika mapambano ya kiroho yanayodaiwa katika maisha ya Kikristo.

 

Post a Comment

Previous Post Next Post