" SKAUTI MANISPAA YA SHINYANGA WAADHIMISHA KUMBUKUMBU YA MWANZILISHI WA SKAUTI DUNIANI, WAZAZI WASISITIZWA KUWARUHUSU WATOTO KUJIUNGA NA SKAUTI

SKAUTI MANISPAA YA SHINYANGA WAADHIMISHA KUMBUKUMBU YA MWANZILISHI WA SKAUTI DUNIANI, WAZAZI WASISITIZWA KUWARUHUSU WATOTO KUJIUNGA NA SKAUTI

Na Mapuli Kitina Misalaba

Chama cha Skauti Manispaa ya Shinyanga leo Jumamos Februari 24,2024 kimeadhimisha kumbukumbu ya mwanzilishi wa Skauti Duniani huku kikiwasihi wazazi na walezi kuwaruhusu watoto kujiunga na chama hicho ili kuendeleza uzalendo wa Taifa.

Skauti hao wa Manispaa ya Shinyanga leo wamefanya matembezi pamoja na kupanda miti zaidia ya Mia moja katika mtaa wa Miti mirefu karibu na Soko la Mboga mboga mjini Shinyanga ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya kumbukumbu ya mwanzilishi wa Skauti Duniani.

Naibu kamishna wa Skauti  Wilaya ya Shinyanga  Mwalimu Veronica Marwa amewataka vijana wa Skauti kuendelea kuziishi kanuni za Skauti kuanzia ngazi ya familia ili kuendeleza Taifa lenye uzalendo.

“Ninawaombeni vijana wangu tuendelee kuziishi kanuni za uskauti tunasema kwamba Skauti ni mwaminifu na ni mtu wa kuaminiwa kwahiyo tuanzia katika ngazi ya familia uaminifu tukiujenga kuanzia ngazi ya familia na jamii kwa ujumla tutatengeneza Taifa lenye uzalendo wa hali ya juu kupitia uzalendo kupitia uzalendo wetu kwa namna mbalimbali kujitoa, kujituma, maadili, uajibikaji tutatengeneza Taifa lenye maendeleo na misingi inayokubalika katika Nchi yetu”.amesema Marwa

Naibu kamishna huyo  Mwalimu Veronica Marwa ametumia nafasi hiyo pia kuwasisitiza vijana kujiepusha kufanya mambo yasiyofaa ambayo hupelekea mmomonyoko wa maadili katika jamii ambapo amewahimiza wanafunzi kusoma kwa bidii huku akiwaomba wazazi na walezi kuwaruhusu watoto kujiunga na Skauti.

“Lika lenu bado mko mashuleni kupitia uskauti wetu naomba tuwe mfano bora kwa wanafunzi wengine tuhakikishe tunasoma kwa bidii kwa sababu ipo imani kwa baadhi ya wazazi wanaona kwamba uskauti huwa una wafanya vijana kuwa wazembe katika masomo yao niwatie moyo tuendelee kupambana darasani tufanye vizuri ili kuondoa hiyo imani ya baadhi ya watu kudhani mnapoteza muda wengine tumeona wenzenu wanazuiwa na wazazi kujiunga kwenye Skauti na kushiriki kwenye shughuli mbalimbali za Skauti, niwaombe wazazi tuwaruhusu watoto kujiunga na Skauti pia tuwaruhusu kushiriki kwenye maadhimisho mbalimbali tunapowahitaji”amesema Marwa.

Aidha Mkufunzi wa Skauti Manispaa ya Shinyanga Ernest Ngaramba ameiomba jamii kuilinda na kuitunza miti iliyopandwa leo na Skauti ili iweze kustawi na vizuri kama sehemu ya kumbukumbu.

“Tumepanda miti ambayo haipungui mia moja hiyo miti tumepanda kwa sababu tunathamini sana umuhimu wa miti katika jamii kwahiyo miti hiyo tuliyoipanda itakuwa na faida sana katika jamii ikiwemo vivuli lakini pia miti inasaidia katika upatikanaji wa mvua, tunachohitaji ni viongozi na jamii inayozunguka eneo hilo kuendelee kuitunza isife”.amesema

Kwa upande wake Mwenyekiti wa mtaa wa miti mirefu ambaye pia ni Mwenyekiti wa wenyeviti Manispaa ya Shinyanga Bwana Nassor Warioba ameahidi kusimamia miti iliyopandwa leo ili iweze kufikia malengo ya serikali kupitia kampeni ya upandaji miti.

“Niwapongeze sana Skauti Manispaa ya Shinyanga kwa kupanda miti siku ya leo na mimi nitahakikisha wanaozunguka eneo hilo wanaitunza ile miti tutashirikia na afisa mazingira kwenda kuwapa utaratibu wa kuitunza ile miti ili iweze kustwi vizuri”.amesema Mwenyekiti Warioba

Chama cha Skauti Manispaa ya Shinyanga kimeungana na watu wengine Duniani kote leo kuadhimisha kumbukumbu ya mwanzilishi wa Skauti Duniani.

Robart Baden Powell ndio jina la muanzilishi wa Skauti Duniani, Alizaliwa Februari 22, 1857 katika mitaa ya Paddington london uingereza.

Robart Baden Powell alikuwa katika jeshi la kiingereza alifanya kazi katika  jeshi hilo mwaka 1876-1910, na kwamba alikuwa na cheo cha liutenant General ambapo Januari 8,1941 alifaliki Dunia akiwa na umri wa Miaka 83 katika jimbo la Nyeri British Kenya.

Skauti ni chama cha hiyari cha kielimu kinachotowa mafunzo kwa vijana wote bila ubaguzi wa rangi,jinsia,dini wala kabila kupitia mafunzo mbalimbali wanayoyapata kwenye mfumo wa vikosi.

Malengo ya Skauti ni kumuandaa kijana kiroho,kimwili,kimtazamo na kijamii ili aweze kujitegemea,kusaidi,kuwajibika na kufaa kwa jamii.

 

 

Matembezi ya Skauti Manispaa ya Shinyanga yakifanyika kama sehemu ya maadhimisho ya kumbukumbu ya mwanzilishi wa Skauti Duniani.


 

Post a Comment

Previous Post Next Post