Na Mapuli Kitina Misalaba
Ligi ya Dumisha Amani imeanza kwa kishindo katika
Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, ikihusisha timu 32 kutoka kata 14, huku
vijana wakihamasishwa kutumia fursa hiyo kuendeleza vipaji na kudumisha amani
nchini.
Uzinduzi rasmi wa ligi
hiyo umefanyika Juni 8, 2025 katika Kata ya Tinde, ukihudhuriwa na wadau
mbalimbali wa michezo, wakiwemo viongozi wa Serikali na Jeshi la Polisi.
Mdhamini mkuu wa ligi
hiyo, Fadhili Nafutari ambaye pia ni mdau mkubwa wa michezo, amewapongeza
waandaaji wa mashindano hayo kwa lengo la kuhamasisha amani, kuibua vipaji na
kusaidia vijana kufikia ndoto zao kupitia soka.
“Nipende kuwaasa kwa
mechi hizi zitakazoendelea kuchezwa kwa timu zote 32, najua wote watafanya vizuri.
Niwaase ndugu zangu vijana, mcheze mpira kwa kujituma. Mpira ni maendeleo,
mpira ni ajira. Mtumie fursa hii vizuri ili mkuze vipaji vyenu muweze kufika
mbali,” amesema Nafutari.
Aidha, amesema michezo
ni daraja la kuunganisha jamii na kufikisha ujumbe wa kudumisha amani, huku
akitoa rai kwa vijana kuitumia Ligi ya Dumisha Amani kama jukwaa la kujitangaza
na kupata nafasi ya kusajiliwa na vilabu vikubwa.
Kwa upande wake,
Mkaguzi Msaidizi wa Jeshi la Polisi ambaye pia ni Polisi Jamii Kata ya Tinde,
Beda Lutego, amesema michezo hiyo ni njia mojawapo ya kuimarisha mshikamano
miongoni mwa wananchi, na pia inaweza kusaidia katika kuwabaini wahalifu
walioko kwenye jamii.
“Tuitumie michezo hii
kuendelea kushirikiana kama jamii, kuimarisha amani na kuwafichua wale wachache
wanaotaka kuivuruga,” amesema Lutego.
Mratibu wa ligi hiyo,
Sungi Leonard amesema mashindano hayo yanahusisha timu kutoka kata 14, na
zitacheza hatua ya makundi hadi kufikia fainali ifikapo Julai 6, mwaka huu 2025.
Baadhi ya wachezaji, wameeleza
kufurahishwa na kuanzishwa kwa ligi hiyo, wakisema ni fursa adimu kwa vijana
kuonyesha uwezo wao mbele ya wadau wa michezo na kupata nafasi ya kutimiza
ndoto zao za kucheza soka la kulipwa.
Ligi ya Dumisha Amani
inaelezwa kuwa mojawapo ya michuano inayosisimua zaidi mwaka huu mkoani
Shinyanga, huku matumaini yakiwa makubwa kwamba itachangia katika kukuza
vipaji, kuleta mshikamano na kudumisha amani katika jamii.


Post a Comment