" KIKUNDI CHA MADEREVA BAJAJI KAGONGWA WAMSHUKURU RAIS MHE. DKT SAMIA SULUHU HASSAN

KIKUNDI CHA MADEREVA BAJAJI KAGONGWA WAMSHUKURU RAIS MHE. DKT SAMIA SULUHU HASSAN

 


Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Mhe. Mboni Mhita (kushoto) pamoja na mkuu wa wilaya ya Kahama Frank Nkinda wakiwa katika moja ya pikipiki za magurudumu matatu (bajaji) za kikundi cha vijanacha madereva wa bajaji Kagongwa, zilizotokana na mapato ya ndani ya Halmashauri ya Manispaa ya Kahama zaidi ya Shilingi milioni 110. Mradi utakaokabidhiwa kwa vijana hao na Mwenge wa Uhuru agosti 3,2025.


Na Mwandishi Wetu - Kahama 

Kikundi cha vijana cha madereva wa pikipiki za magurudumu matatu (bajaji) kilichonufaika na mikopo ya 10% iliyotolewa na Halmashauri ya Manispaa ya Kahama mkoani Shinyanga, kimeishukuru serikali kwa kuwapatia mkopo huo, na kwamba utawasaidia kujikwamua kiuchumi.

 

Wametoa shukrani hizo, wakati wa ziara ya mkuu wa mkoa huo Mhe. Mboni Mhita, iliyolenga kupitia, kuona na kukagua miradi ya Mwenge wa Uhuru 2025 katika Manispaa ya Kahama.

 

Wamesema “Shukrani zetu za dhati kabisa tunazipeleka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan, kwa kutuhakikishia vijana amani na Uchumi wa uhakika, haswa kwa mikopo hii ya 10%, na sisi tunamuunga mkono kwa juhudi hizi”

 

“Rais wetu ana moyo wa tofauti, kwa mfano kama sisi hizi fedha hatujawahi hata kuwaza kuzishika, ila leo tumezishika tena bila riba. Tumepewa milioni 110, tunarudisha milioni 110, hakuna riba, kweli ni moyo mwema sana. Tulizoea mikopo umiza huko mtaani ambayo sasa tumeiepuka kabisa. Oktoba tunatiki” Na kuongeza

 

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Shinyanga Mhe. Mboni Mhita, amewahakikishia vijana mkoani humo kuwa, serikali inawathamini na kuuangalia Uchumi wao kila kukicha kuhakikisha unakua, na kwamba mikopo hiyo itaendelea kutolewa katika kila Halmashauri mkoani humo.

 

“Serikali inafahamu changamoto zenu, na mikopo hii inatoka kwa Mhe. Rais Dr Samia Suluhu Hassan ambaye ameelekeza kila Halmashauri kutenga na kutoa 10% ya mapato yake ya ndani kwa ajili ya 4% kwa vijana, 4% kwa wanawake na 2% kwa watu wenye ulemavu” Amesema Mhe. Mboni

 

Mradi wa kikundi cha vijana cha madereva pikipiki za magurudumu matatu (bajaji) kilichopo kata ya Kagongwa, Manispaa ya Kahama, katika Mbio za Mwenge wa Uhuru 2025, kitakabidhiwa pikipiki 10 zenye thamani ya zaidi ya Shilingi milioni 110, ambazo ni mapato ya ndani ya Halmashauri hiyo.

 

Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, imekuwa ikitenga na kutoa 10% ya mapato yake ya ndani Kwenda kwa wanawake, vijana na wenye ulemavu, ambapo katika robo ya nne ya mwaka 2024/2025, zaidi ya Shilingi Bilioni 1.2 zilitolewa kwa makundi hayo, kikiwemo kikundi cha vijana cha madereva wa pikipiki za magurudumu matatu Kagongwa (bajaji).

 

 Aidha Halmashauri ya Manispaa ya Kahama mkoani Shinyanga, inatarajiwa kuupokea Mwenge wa Uhuru 2025, kimkoa Agosti 3, 2025 ukitokea mkoani Tabora, na kuanza kukimbizwa siku hiyo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama.

 

 Mwenge wa Uhuru 2025, utapokelewa katika viwanja vya kituo cha mabasi Kagongwa ukitokea Tabora majira ya saa 12 kamili asubuhi ambapo wananchi wote wanakaribishwa kushuhudia zoezi hilo.

 

 Mkesha wa Mwenge wa Uhuru katika Manispaa hiyo August 3, 2025, ni katika uwanja wa Magufuli ambapo shughuli mbalimbali za kijamii zitakuwa zikiendelea ikiwemo upimaji wa ugonjwa wa malaria bure kwa wananchi wote.

 

 Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu 2025, zinabeba kauli mbiu isemayo “Jitokeze Kushiriki Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 kwa Amani na Utulivu”.


Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Mhe. Mboni Mhita aliyevaa blauzi nyeusi, akikagua akikagua Mradi wa ujenzi wa chujio la maji Mwendakulima wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 2.87, utakaowekewa jiwe la msingi na Mwenge wa Uhuru mwaka huu 2025. 


Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Mhe. Mboni Mhita akishuhudia masomo ya sayansi kwa vitendo kwenye maabara ya kisasa ya sayansi mchanganyiko katika shule ya sekondari mama Kalembe, kata ya Mwendakulima, Manispaa ya Kahama, iliyogharimu zaidi ya shilingi milioni 58.3, ambao unatarajiwa kufunguliwa na Mwenge wa Uhuru 2025.


Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Mhe. Mboni Mhita akizungumza wakati wa ukaguzi wa Mradi wa ujenzi wa jengo la uraibu wa dawa za kulevya katika Hospitali ya Manispaa ya Kahama wenye thamani ya zaidi ya Shilingi milioni 349.8.




Post a Comment

Previous Post Next Post