" MADEREVA WA MAGARI YA ABIRIA WAPATIWA ELIMU YA USALAMA BARABARANI KUHUSU VIVUKO VYA RELI

MADEREVA WA MAGARI YA ABIRIA WAPATIWA ELIMU YA USALAMA BARABARANI KUHUSU VIVUKO VYA RELI

Madereva wa magari ya abiria wamepatiwa elimu ya usalama barabarani, hususani ulazima wa kusimama kwenye vivuko vya reli ili kujikinga na ajali zisizo za lazima na kulinda maisha ya abiria wanaowasafirisha.

Elimu hiyo imetolewa na Askari Polisi wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Shinyanga, Sajenti David Ndimila, wakati akizungumza na madereva hao ambapo amewataka kuacha mazoea ya kupita kwenye vivuko vya reli pasipo kuchukua tahadhari.

Amesema kuwa ni muhimu kwa madereva kusimama na kujihakikishia usalama kabla ya kuvuka reli ili kuepusha ajali zinazoweza kutokea ikiwemo kugongwa na gari moshi.

“Kabla ya kuvuka reli, dereva anatakiwa kusimama, kuhakikisha hakuna gari moshi linalokuja, kisha kuendelea na safari. Tabia ya kupuuza sheria hii imekuwa chanzo cha ajali nyingi ambazo zingeweza kuepukika,” amesema Sgt Ndimila.

Aidha, amewaasa madereva wa magari ya abiria kuwa mfano bora wa kuigwa na madereva wengine kwa kufuata sheria za usalama barabarani, ili kuhakikisha abiria wanaosafirishwa wanawasili salama kwenye safari zao na pia kuepuka majanga yanayoweza kuhusisha treni.

Sajenti Ndimila amesisitiza kuwa elimu ya usalama barabarani ni jukumu la kila dereva, na kufuata masharti ya usalama kwenye vivuko vya reli ni hatua muhimu ya kupunguza ajali na kulinda maisha ya wananchi.

 


 

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

Post a Comment

Previous Post Next Post