" MKUTANO WA DP SHINYANGA WAAHIRISHWA KUFUATIA KAULI TATA ZA MAKAMU MWENYEKITI ZANZIBAR

MKUTANO WA DP SHINYANGA WAAHIRISHWA KUFUATIA KAULI TATA ZA MAKAMU MWENYEKITI ZANZIBAR

 


Mgombea Urais kupitia Chama cha Democratic Party (DP), Abdul Juma Mluya, akizungumza na waandishi wa habari wilayani Kahama leo septemba 26 baada ya kuahirishwa kwa mikutano ya kampeni iliyokuwa imepangwa kufanyika wilayani Kahama na katika manispaa ya Shinyanga kwa nyakati tofauti, kutokana na kuzorota kwa hali yake ya kiafya.

Na Neema Nkumbi, Kahama


Mikutano ya kampeni ya Mgombea Urais kupitia Chama cha Democratic Party (DP), Abdul Juma Mluya, iliyopangwa kufanyika mkoani Shinyanga, kwa nyakati tofauti, imeahirishwa ghafla kutokana na hali mbaya ya kiafya ya mgombea huyo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo baada ya kuahirishwa kwa mkutano wa kampeni uliokuwa ufanyika katika kata ya Mhongolo manispaa ya Kahama, Mluya amesema kuzorota kwa afya yake kumesababishwa na sintofahamu ya kauli ya Makamu Mwenyekiti wa chama hicho upande wa Zanzibar, Peter Agaton Magwira.


"Makamu mwenyekiti wa chama chetu kwa upande wa Zanzibar, jana ametoa kauli kwamba eti, chama kimekaa na kukubaliana kumuunga mkono mgombea urais Zanzibar kupitia Chama cha Mapindizi (CCM). Amesema Mluya na kuongeza kuwa

"Kauli hiyo ni ya kwake, na sio ya chama chetu. Mimi kama mgombea na mwenyekiti wa chama, kauli hiyo imeniathiri sana kiafya, imeniletea mshtuko wa moyo na nimeshindwa kuendelea na mikutano ya kampeni iliyokuwa imeandaliwa ukiwemo huu wa Kahama na kesho Shinyanga."


Amesisitiza kuwa hakuna kikao rasmi cha chama kilichokaa na kutoa msimamo huo, hivyo kauli ya Magwira si msimamo wa DP bali ni maoni binafsi, huku akirejea Katiba ya chama hicho ibara ya 13(2), inayoeleza kuwa mwenyekiti ndiye msemaji na mlinzi wa katiba ya chama, hivyo taarifa ya makamu mwenyekiti inapaswa kupuuzwa.

Aidha amemuagiza Katibu Mkuu wa DP kuandaa barua ya kumsimamisha kwenye nafasi yake Peter Agaton Magwira, baadhi ya wanachama na wajumbe saba wa sekretarieti waliokuwa sehemu ya mkutano huo.

wajumbe hao ni Leonard Mkoga, Makame Omary Makame, Mariam Maseka, Juma Kidawa, Salma Mateo, Mkude John Mkude na Zainabu Khamis.

Barua hizo zitatumika kupeleka mashauri yao katika Kamati ya Maadili, kisha kufikishwa kwenye Mkutano Mkuu ili wajitete na kuamuliwa adhabu stahiki, kuanzia onyo, kusimamishwa, au hata kufutwa uanachama.

Hata hivyo, licha ya kadhia hiyo, Mluya amewahakikishia Watanzania kuwa ataendelea kusimama kama mtetezi wa walala hoi, huku akisisitiza chama chake hakitapoteza mwelekeo wa awali wa kampeni.

Ratiba mpya ya mikutano ya Kahama na Shinyanga inatarajiwa kupangwa na kamati husika baada ya tathmini ya afya yake.

Ametoa wito kwa watanzania kudumisha amani, upendo na mshikamano katika kipindi hiki cha kampeni za kuelekea uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani, huku akiwasihi wanasiasa kufanya kampeni za kistaarabu na kushindana kwa hoja.



“Hakuna chama chenye haki miliki ya Tanzania, Kama ingekuwa hivyo, basi kusingekuwa na sababu ya kuendesha uchaguzi, kwa hiyo tunadi sera zetu, tushindane kwa hoja.”

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

Post a Comment

Previous Post Next Post