" WALIMU WANAWAKE MANISPAA YA SHINYANGA WAJENGEWA UWEZO KUIMARISHA UONGOZI, UCHUMI NA MAADILI KAZINI

WALIMU WANAWAKE MANISPAA YA SHINYANGA WAJENGEWA UWEZO KUIMARISHA UONGOZI, UCHUMI NA MAADILI KAZINI

Walimu wanawake wa Manispaa ya Shinyanga wamehimizwa kuendeleza umoja, mshikamano na weledi katika kazi zao ili kuimarisha ubora wa elimu na kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi kupitia taaluma yao.

Kauli hiyo imetolewa katika kongamano la walimu wanawake wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) Manispaa ya Shinyanga, lililofanyika Oktoba 24, 2025, likiwa na lengo la kuwajengea uwezo katika nyanja za uongozi, uchumi, sheria na ustawi wa jamii.

Kongamano hilo limeandaliwa na Kitengo cha Walimu Wanawake Manispaa ya Shinyanga chini ya uongozi wa Mwenyekiti Mwl. Subira Mustafa Kuhenga, kwa ushirikiano na Mwenyekiti wa upande wa KE Rose Mabana na Mweka Hazina Stella Halimoja.

Katika kongamano hilo, mada mbalimbali zimejadiliwa ikiwemo Sheria ya Ndoa, Mirathi na Talaka, Mahusiano Kazini, Uchumi na Mikopo yenye masharti nafuu, Ujasiriamali, Uongozi wa Mwanamke na Mapambano dhidi ya Ukatili wa Kijinsia.

Akizungumza wakati wa kikao hicho, Afisa Utumishi wa Manispaa ya Shinyanga, Bw. Jackson Mwakisu, amesema mwalimu mwanamke ana nafasi kubwa katika kulilea jamii na kujenga uchumi wa familia, hivyo ni muhimu kuwekeza katika mafunzo yatakayowasaidia kuwa viongozi bora, wachapakazi na wenye dira.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Walimu Manispaa ya Shinyanga, Mwl. Subira Mustafa Kuhenga, amesema lengo la makongamano hayo ni kuhakikisha walimu wanawake wanapata elimu ya kujitambua, kujenga kujiamini na kuimarisha ushirikiano katika kazi na jamii.

Ameongeza kuwa kongamano hilo limekuwa jukwaa la kuunganisha walimu katika kujadili changamoto zinazowakabili na kuzitafutia suluhisho la pamoja.

Aidha, Mwanasheria Ruth Ndagu, akiwasilisha mada ya Sheria ya Ndoa na Mirathi, amesema ni muhimu kwa walimu wanawake kuelewa haki zao za kisheria ili kuepuka kudhulumiwa katika mali, mirathi au ndoa, na kuwaelimisha wanafunzi wao juu ya haki na wajibu katika jamii.

Katika hatua nyingine, Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake Laki Moja Mkoani Shinyanga, Bi. Anascolastica Ndagiwe, amewataka walimu wanawake kutumia utu na weledi wao kupinga ukatili wa kijinsia mashuleni, akisisitiza kuwa mwalimu ndiye nguzo muhimu ya kumlinda mtoto dhidi ya manyanyaso na malezi yasiyo bora.

Naye Katibu wa Kitengo cha Walimu Wanawake Taifa, Bi. Elizabeth Werema, amesema mapambano dhidi ya ukatili hayaanzi shuleni pekee bali nyumbani, hivyo kila mwalimu anatakiwa kuwa kioo cha maadili, malezi na heshima kwa jamii.

Mjumbe wa Kamati Tendaji ya CWT Taifa, Bi. Grace Kulwa, amebainisha kuwa kongamano hilo limekuwa fursa kwa walimu wanawake kubadilishana uzoefu, kujifunza mbinu za kuimarisha mahusiano kazini, na kuongeza kipato kupitia miradi ya ujasiriamali na uwekezaji.

Akihitimisha kongamano hilo, Mwenyekiti wa Kitengo cha Walimu Wanawake Taifa, Bi. Neema Obedi, amesema mafunzo hayo yatasaidia kujenga kizazi cha walimu wanawake wenye uelewa mpana, wanaoweza kulea kizazi cha wanafunzi wachapa kazi, wenye nidhamu na uzalendo.

 Mwenyekiti wa upande wa KE Rose Mabana, akizungumza.

 Mwenyekiti wa upande wa KE Rose Mabana, akisoma risala ya walimu wanawake Manispaa ya Shinyanga.






 

Post a Comment

Previous Post Next Post