" TAKUKURU SHINYANGA YAOKOA VIFAA VYA UJENZI VYENYE THAMANI YA SH MILIONI 51.7 KATIKA UFUATILIAJI WA MIRADI YA MAENDELEO

TAKUKURU SHINYANGA YAOKOA VIFAA VYA UJENZI VYENYE THAMANI YA SH MILIONI 51.7 KATIKA UFUATILIAJI WA MIRADI YA MAENDELEO

Na Mapuli Kitina Misalaba

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Shinyanga imefanikiwa kuokoa vifaa vya ujenzi vyenye thamani ya Shilingi 51,752,600 kufuatia ufuatiliaji wa matumizi ya fedha za utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika Halmashauri za Mkoa wa Shinyanga.

Akizungumza wakati wa kutoa taarifa kwa vyombo vya habari, Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga, Donasian Kessy, amesema hatua hiyo imechukuliwa baada ya kubainika kuwa mzabuni wa mradi wa ujenzi wa nyumba ya mtumishi katika Shule ya Msingi Magongwa, Halmashauri ya Wilaya ya Msalala, alinunua vifaa vya ujenzi lakini hakuvifikisha kwenye eneo la mradi.

Vifaa vilivyookolewa ni pamoja na nondo, vigae (25x40), vifaa vya umeme, vifaa vya maji, vyoo, gypsum board na rangi. Kufuatia ufuatiliaji huo, TAKUKURU ilimtaka mzabuni kuwasilisha mara moja vifaa hivyo katika mradi husika ili kuhakikisha thamani ya fedha za umma inalindwa.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, katika kipindi cha Oktoba hadi Desemba 2025, TAKUKURU imefuatilia jumla ya miradi 18 ya maendeleo yenye thamani ya Shilingi 3,536,123,370 katika Mkoa wa Shinyanga.

Ufuatiliaji huo umeelezwa kuwa ni sehemu ya mkakati wa kuimarisha uwajibikaji, kuzuia ubadhirifu wa fedha za umma na kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa viwango vinavyokusudiwa kwa manufaa ya wananchi.

TAKUKURU imewataka watendaji wa umma na wazabuni kuzingatia mikataba na taratibu za ununuzi ili kuepusha hatua za kisheria, huku wananchi wakihimizwa kuendelea kutoa taarifa za vitendo vya rushwa au ubadhirifu kupitia namba 113 bure.

  

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment

Previous Post Next Post